SIMBA SC KWAZIDI KUWAKA, HANSPOPPE ABWAGA MANYANGA


HALI ndani ya klabu ya soka ya Simba imezidi kuwa  mbaya baada ya mjumbe wa kamati ya Utendaji na Mwenyekiti wa Kamati ya usajili ya Zacharia Hans Poppe kujiuzulu. 
Hatua hiyo inafuatia timu hiyo kufanya vibaya katika michezo yake ya ligi kuu ya Vodacom, pamoja na kutolewa katika raundi ya kwanza kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika na Recreativo do Libolo ya Angola wiki iliyopita kwa jumla ya mabao 5-0. 
Habari za uhakika kutoka ndani ya klabu ya Simba zinaeleza kwamba, mara baada ya kutolewa kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika,  Poppe ambaye pia ni mwenyekiti wa kundi la marafiki wa Simba ‘Friends of Simba’ alisema atatoa uamuzi mzito. 
Kiongozi mmoja wa Simba amesema leo  kwamba, Poppe alishindwa hata kuhudhuria kikao cha kamati ya utendaji ya Simba pamoja na wadhamini wa klabu hiyo kilichofanyika jana usiku kwa ajili ya kujadili ripoti ya timu hiyo baada ya mchezo wake wa Libolo. 
Alisema Poppe hakutoa sababu zozote za kutohudhuria kikao hicho ambacho baada ya kupokea ripoti ya kamati ya utendaji kiliijadili na kutoa uamuzi wake. 
Poppe ambaye tayari ameshawasilisha barua ya kujiuzulu kwake jana kwa uongozi wa Simba kwa akidai kusikitisha na sintofahamu inayoendelea ndani ya klabu hiyo, hivyo kuamua kujiweka kamndo na kubaki kuwa mwanachama mwaminifu wa klabu hiyo yenye maskani yake mitaa ya Msimbazi na Twiga. 
Mwandishi wa habari hizi alipomtafuta Poppe kwa ajili ya kuthibitisha taarifa hizi simu yake iliita bila majibu, huku Katibu wa Simba Evodius Mtawala naye simu yake iliita bila kupokelewa. 
Hivi karibuni hali ndani ya klabu ya Simba imezidi kuwa ‘tete’  ambapo kumekuwepo na shinikizo la wanachama wa klabu hiyo kumtaka mwenyekiti wa klabu hiyo, Alhajj Ismail Aden kumtaka ajiuzulu kwa madai ya kushindwa kuiongoza vema klabu hiyo. 
Hata hivyo Rage amekuwa akikwepa shinikizo hilo kwa madai kwamba wanaocheza ni wachezaji si viongozi na kwamba hawezi kujiuzulu kwa ajili ya shinikizo la watu wachache na kama atafikia uamuzi wa kufanya hivyo, atatangaza kwenye mkutano wa wanachama. 
Kama hiyo haitoshi, kamati ya utendaji ya Simba iliyokutana wiki iliyopita ilitangaza kuitishwa kwa mkutano mkuu wa dharala kwa ajili ya kujadili mustakabali wa timu hiyo, lakini kuna taarifa kuwa Rage amekuwa akipinga kufanyika kwa mkutano mkuu wa dharula, yote ni katika kuhofia kupinduliwa. 
Aidha, kuna taarifa zinabainisha kuwa, kufanya vibaya kwa Simba katika michezo yake kunatokana na mgomo bairidi unaofanywa na wachezaji wa timu hiyo ambao wanapinga kubaguliwa na makocha wa timu hiyo pamoja na baadhi ya viongozi. 
Simba ambayo kwa sasa inashika nafasi ya tatu ikiwa na pointi 31 imeshauweka rehani ubingwa wake ambapo sasa Yanga inayoongoza ligi hiyo  kwa pointi 42 na Azam Fc inayoshika nafasi ya pili ikiwa na pointi  36 ndizo zinazochuana katika kuwania ubingwa wa ligi hiyo.

Comments