WANACHAMA zaidi ya 700 wa klabu ya soka ya Simba wameung’oa
uongozi wa klabu hiyo chini ya mwenyekiti wake, Alhaj Ismail Aden Rage.
Katika mkutano huo ukliofanyika kwenye hoteli ya Starlight
wamekubaliana kwa kauli moja kuundoa uongozi huo na kukasimu madaraka kwa
Zacharia Hanspoppe na Rahma Al Kharoos kuongoza kwa muda mpaka ligi
itakapokamilika.
Mkutano huo ambao
ulibeba ajenda ya kujadili mwenendo wa
klabu hiyo kwenye Ligi Kuu ya Soka ya Tanzania Bara ambapo wanachama hao
walieleza kutokuwa na imani na uongozi wa klabu hiyo kwa madai kuwa timu haifanyi vizuri kwenye ligi na mashindano ya
kimataifa, usajili mbovu na kudanganywa mara kwa mara na mwenyekiti huyo na
wajumbe wa kamati ya utendaji ya klabu hiyo kwenye mambo mbalimbali ikiwemo suala la kujenga uwanja.
Akizungumza kwenye mkutano huo Mwenyekiti wa Mkutano huo
Mohamedi Wandwe alisema kuwa Hans Pope na Rahma Al Kharoos watateua wajumbe wa
kuwasaidia na wataitisha Mkutano Mkuu wa Uchaguzi baada ya Ligi Kuu ya Soka ya
Tanzania Bara kumalizika.
“Ibara ya 16(g) ya Katiba ya klabu ya Simba inatoa mamlaka
ya mkutano huu kuunda chombo kitakachosimamia kuanzia kesho mpaka uchaguzi
utakapofanyika, na tumewachagua Zakaria Hans Pope na Rahma Al Kharoos kuongoza
kamati ya muda ya Simba mpaka ligi itakapomalizika,”alisema Wandwe.
Alisema kuwa Katiba ya Simba inatoa muda wa siku 90
kuitishwa kwa Mkutano Mkuu wa Uchaguzi lakini kwa kuwa ligi bado inaendelea wameipa
Kamati ya muda mpaka ligi itakapomalizika kuitisha Mkutano Mkuu wa Uchaguzi
huku kesho wakitarajia kupeleka kwa msajili wa vyama na Shirikisho la Soka Tanzania(TFF) mabadiliko hayo ya uongozi ili yatambulike na mamlaka hizo husika.
Kwa upamnde wake Shirikisho la Soka nchini(TFF) kupitia kwa
msemaji wake Boniface Wambura lilisema kwenye Katiba ya shirikisho hilo na katiba
ya klabu ya Simba hakuna kitu kinachoitwa uongozi wa kamati ya muda hivyo
mabadiliko hayo ya uongozi ni batili.
Alisema kwa mujibu wa Katiba ya Simba Mkutano Mkuu wa
wanachama unaitishwa na Mwenyekiti wa klabu na sio mtu mwingine yoyote.
Wambura alisema wanachama wa Simba wanaweza kufanya mambo
mawili kama hawautaki uongozi uliopo madarakani na kutaja mambo hayo kuwa ni
kuorodhesha idadi ya wanachama na ikitimia 500 wapeleke kwa Kamati ya
Utendaji ya klabu hiyo kwa ajili ya kuitisha Mkutano Mkuu wa wanachama ambapo
watapata nafasi ya kuelezea kutokuwa na imani na viongozi wao.
Hatua nyingine Wambura alisema ni kwa wajumbe wengi wa
Kamati ya Utendaji iliyopo madarakani kujiuzulu ili kumshinikiza Mwenyekiti wa klabu hiyo kuitisha Mkutano
Mkuu wa Uchaguzi, kinyume cha hayo ni sawa na kupoteza muda.
Akizungumzia hatua hiyo, Mwenyekiti wa Matawi ya klabu ya
Simba Ramadhani Khamisi’ Don King’ alisema kuwa Mkutano huo ni batili na hauwakilishi wanachama wa klabu hiyo bali wanachama wa tawi la mpira pesa na kuongeza
kuwa mwenye malaka ya kuitisha mkutano mkuu ni mwenyekiti ambaye kwa sasa yupo
nchini india kwa matibabu..
Don King pia ameshangazwa na wanachama hao kwa kuwateua Hans
Pope na Rahma Al Kharoos na kusema kama wanampinga Rage, hawana budi kuwapinga
Hanspoppe ambaye alifanya kazi chini ya rage na AL Kharoos aliletwa na Rage kutoka Oman.
“Kama wanampinga Rage, wampinge pia na Hans Pope kwani nae
alikuwa kiongozi wa Simba na alishiriki kwa kiasi kikubwa kwenye usajili
wanaosema ni mbovu na watambue kuwa ni Rage aliyemleta Al Kharoos kutoka Oman,
sasa iweje leo wampinge,”alihoji Khamisi.
Khamsi alisema yeye kama Mwenyekiti wa Matawi ya Simba Dar
es Salaam anauchukulia mkutano huo ni wa kihuni na uliofanywa na watu
wasioielewa katiba ya klabu hiyo.
Comments
Post a Comment