RAGE APINDULIWA RASMI,HANSPOPPE, ALKHAROOS KUONGOZA:TFF HAIWEZEKANI


WANACHAMA zaidi ya 700 wa klabu ya soka ya Simba wameung’oa uongozi wa klabu hiyo chini ya mwenyekiti wake, Alhaj Ismail Aden Rage.
Katika mkutano huo ukliofanyika kwenye hoteli ya Starlight wamekubaliana kwa kauli moja kuundoa uongozi huo na kukasimu madaraka kwa Zacharia Hanspoppe na Rahma Al Kharoos kuongoza kwa muda mpaka ligi itakapokamilika.
 Mkutano huo ambao ulibeba ajenda ya  kujadili mwenendo wa klabu hiyo kwenye Ligi Kuu ya Soka ya Tanzania Bara ambapo wanachama hao walieleza kutokuwa na imani na uongozi wa klabu hiyo kwa madai kuwa timu  haifanyi vizuri kwenye ligi na mashindano ya kimataifa, usajili mbovu na kudanganywa mara kwa mara na mwenyekiti huyo na wajumbe wa kamati ya utendaji ya klabu hiyo kwenye mambo mbalimbali ikiwemo  suala la kujenga uwanja.
Akizungumza kwenye mkutano huo Mwenyekiti wa Mkutano huo Mohamedi Wandwe alisema kuwa Hans Pope na Rahma Al Kharoos watateua wajumbe wa kuwasaidia na wataitisha Mkutano Mkuu wa Uchaguzi baada ya Ligi Kuu ya Soka ya Tanzania Bara kumalizika.
“Ibara ya 16(g) ya Katiba ya klabu ya Simba inatoa mamlaka ya mkutano huu kuunda chombo kitakachosimamia kuanzia kesho mpaka uchaguzi utakapofanyika, na tumewachagua Zakaria Hans Pope na Rahma Al Kharoos kuongoza kamati ya muda ya Simba mpaka ligi itakapomalizika,”alisema Wandwe.
Alisema kuwa Katiba ya Simba inatoa muda wa siku 90 kuitishwa kwa Mkutano Mkuu wa Uchaguzi lakini kwa kuwa ligi bado inaendelea wameipa Kamati ya muda mpaka ligi itakapomalizika kuitisha Mkutano Mkuu wa Uchaguzi huku kesho wakitarajia kupeleka kwa msajili wa vyama na Shirikisho la Soka Tanzania(TFF) mabadiliko hayo ya uongozi ili yatambulike na mamlaka hizo husika.
Kwa upamnde wake Shirikisho la Soka nchini(TFF) kupitia kwa msemaji wake Boniface Wambura lilisema kwenye Katiba ya shirikisho hilo na katiba ya klabu ya Simba hakuna kitu kinachoitwa uongozi wa kamati ya muda hivyo mabadiliko hayo ya uongozi ni batili.
Alisema kwa mujibu wa Katiba ya Simba Mkutano Mkuu wa wanachama unaitishwa na Mwenyekiti wa klabu na sio mtu mwingine yoyote.
Wambura alisema wanachama wa Simba wanaweza kufanya mambo mawili kama hawautaki uongozi uliopo madarakani na kutaja mambo hayo kuwa ni kuorodhesha idadi ya wanachama na ikitimia 500 wapeleke kwa Kamati ya Utendaji ya klabu hiyo kwa ajili ya kuitisha Mkutano Mkuu wa wanachama ambapo watapata nafasi ya kuelezea kutokuwa na imani na viongozi wao.
Hatua nyingine Wambura alisema ni kwa wajumbe wengi wa Kamati ya Utendaji iliyopo madarakani kujiuzulu ili kumshinikiza  Mwenyekiti wa klabu hiyo kuitisha Mkutano Mkuu wa Uchaguzi, kinyume cha hayo ni sawa na kupoteza muda.
Akizungumzia hatua hiyo, Mwenyekiti wa Matawi ya klabu ya Simba Ramadhani Khamisi’ Don King’ alisema  kuwa Mkutano huo ni batili na  hauwakilishi wanachama wa klabu hiyo bali  wanachama wa tawi la mpira pesa na kuongeza kuwa mwenye malaka ya kuitisha mkutano mkuu ni mwenyekiti ambaye kwa sasa yupo nchini india kwa matibabu..
Don King pia ameshangazwa na wanachama hao kwa kuwateua Hans Pope na Rahma Al Kharoos na kusema kama wanampinga Rage, hawana budi kuwapinga Hanspoppe ambaye alifanya kazi chini ya rage na  AL Kharoos aliletwa na Rage kutoka Oman.
“Kama wanampinga Rage, wampinge pia na Hans Pope kwani nae alikuwa kiongozi wa Simba na alishiriki kwa kiasi kikubwa kwenye usajili wanaosema ni mbovu na watambue kuwa ni Rage aliyemleta Al Kharoos kutoka Oman, sasa iweje leo wampinge,”alihoji Khamisi.
Khamsi alisema yeye kama Mwenyekiti wa Matawi ya Simba Dar es Salaam anauchukulia mkutano huo ni wa kihuni na uliofanywa na watu wasioielewa katiba ya klabu hiyo.



Comments