MWENYEKITI wa klabu ya Simba ya jijini Dar es Salaam, Ismail
Aden Rage, amekiri nafasi ya kikosi chake kutetea ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania
Bara ni finyu hasa kutokana na aina ya matokeo mabovu inayovuna katika
mfululizo wa ligi hiyo.
Rage aliyasema hayo mara baada ya Wekundu wa Msimbazi Simba
kukubali kichapo cha ugenini cha bao 1-0 kutoka kwa Kagera Sugar kwenye Uwanja
wa Kaitaba, mjini Bukoba juzi, matokeo yaliyozidi kuididimiza timu hiyo, wakati
alipokuwa akihojiwa na kipindi cha Spoti Leo cha Radio One.
Watetezi hao wameendelea kubaki katika nafasi ya tatu ya
msimamo wa ligi hiyo, wakiwa na pointi 34, sita nyuma ya Azam FC inayoshika
nafasi ya pili, huku Yanga ikiongoza kwa pointi 48.
Rage katika kile kilichoonekana kama
‘kukubali matokeo’, alisema sio lazima kila mwaka bingwa wa ligi hiyo akawa
Simba, hasa kutokana na ushindani mkubwa uliopo miongoni mwa timu shiriki 14 za
Tanzania Bara.
“Kama tunataka kuchukua
ubingwa kila mwaka, basi tungeunda ligi yetu ambayo ingekuwa na timu tano za
Simba ili kila mwaka tuwe mabingwa sisi wenyewe. Lakini hatuwezi kutwaa ubingwa
kila mwaka kwa kuwa kuna timu nyingi zinazouwania,” alisema Rage.
Katika msisitizo wake, Rage alisema kufuatia matokeo hayo ya
Simba hawezi kujiuzulu, kwa kuwa aliahidi kuijenga Simba imara ambapo alisema
atashirikiana na viongozi wenzake katika kuhakikisha hali inakuwa shwari na
timu inafanya vizuri tena.
“Mimi si kocha wala sio mchezaji. Kwani mimi ni beki? Kwa
hiyo mkiniuliza habari za matokeo mabovu siwezi kuwaambia lolote, zaidi ya
ukweli kuwa ni hali ya mchezo ambao una matokeo ya kushinda, kupoteza au sare,”
alisisitiza Rage.
Aidha alibainisha kuwa anajipanga kuweka mambo sawa kuhusu
hatima ya mgogoro baina yake na baadhi ya wanachama, ambao baadhi yao hivi karibuni walitangaza kuupindua uongozi wake
wakati akiwa kwenye matibabu nchini India .
“Leo nilishindwa kufanya mkutano na waandishi wa habari
kutokana na kujisikia vibaya maana bado hali ya afya yangu tangu nitoke
hospitali haijaimarika, lakini nitakapokuwa tayari nitatoa taarifa,” alisema
Rage.
Comments
Post a Comment