MNYAMA CHALI KAITABA, KANONI ATOA PASI YA BAO LA KIFO CHA SIMBA




Kikosi ncha Kagera, Amandus Nesta wa pili kutoka kushoto waliosimama

Na Asha Said, Bukoba
MNYAMA chali Kaitaba. Naam, Wekundu wa Msimbazi leo wameshindwa kufurukuta mbele ya Kagera Sugar, baada ya kuchapwa bao 1-0 kwenye Uwanja wa Kaitaba, Bukoba jioni hii.
Matokeo hayo yanzidi kupoteza matumaini ya Simba SC japo kucheza michuano ya Kombe  la Shirikisho Afrika mwakani, wakiwa wanazidiwa pointi sita sasa na Azam FC (40-34) inayoshika nafasi ya pili. Yanga inaongoza kwa pointi zake 48. 
Hadi mapumziko hakuna timu iliyokuwa imefanikiwa kupata bao na Kagera Sugar ndio waliocheza vizuri zaidi na kukaribia kufunga mara mbili. 
Kwanza ilikuwa dakika ya tano, baada ya Jumanne Daudi kumjaribu ‘Tanzania One’, Juma Kaseja lakini shuti lake likapaa juu ya lango na baadaye dakika ya 22 Juma Nade alitaka kutumia vema makosa ya beki Shomary Kapombe kuchelewa kuokoa, lakini akapiga fyongo.
Kipindi cha pili Kagera Sugar inayofundishwa na gwiji wa zaman wa SImba SC, ABdallah Kibadeni, iliingia na kasi  ya kutosha na kufanikiwa kupata bao la mapema tu dakika ya kwanza.  
Alikuwa ni beki Amandus Nesta aliyefanikiwa kufunga bao hilo dakika ya 46 akiunganisha kwa kichwa kona iliyochongwa na beki wa zamani wa Simba SC, Salum Kanoni Kupela. 
Simba SC; Juma Kaseja, Nassor Masoud ‘Chollo’, Miraj Adam, Hassan Khatibu, Shomary Kapombe, Jonas Mkude, Edward Christopher, Abdallah Seseme, Mrisho Ngassa, Ramadhan Singano ‘Messi’ na Haruna Chanongo.
Kagera Sugar; Andrew Ntala, Benjamin Asukile, Salum Kanoni, Benjamin Effe, Amandus Nesta, Malegesi Mwangwa, Juma Mpola, Juma Nade, Jumanne Daudi, Darington Enyinna na Paul Ngway.
CHANZO:Bongostaz blog

Comments