KLABU ya Etoile du Sahel
ya Tunisia, imewataka viongozi wa klabu ya Simba kuvuta subira kuhusu malipo ya
mchezaji Emmanuel Okwi aliyejiunga na wakali hao mapema mwaka huu.
Kwa mujibu wa barua ya
Machi 13, mwaka huu, iliyosainiwa na Katibu Mkuu wake Adel Ghith, kukawia kwa
malipo ya nyota huyo wa kimataifa wa Uganda, ni kutokana na matizo ya taratibu
za kibenki katika
kuhamisha fedha kutoka benki kuu ya nchi hiyo kuja Tanzania.
“Kwako mwenyekiti,
tumekuwa tukifanya jitihada kubwa za kuhamisha fedha kutoka Benki Kuu ya hapa
(Tunisia), kumekuwa na vikwazo vya kiuchumi na kisiasa, tutajitahidi kufanya
kila tuwezalo kupata nyaraka muhimu Benki Kuu,” ilisema sehemu ya barua hiyo.
Adel alijinasibu kuwa kwa
hadhi ya klabu yao ambayo kwa miaka 20 sasa imekuwa na wastani wa nyota watatu
kila msimu, haiwezi kufanya hila kwenye jambo hilo la Okwi kwa maslahi ya pande
zote mbili.
Kiongozi huyo aliongeza
kuwa changamoto za kisiasa na kiuchumi ambazo nchi ya Tunisia inapitia kwa
sasa, kwa upande mwingine zinawafanya viongozi wa klabu hiyo kujituma zaidi kwa
maslahi ya klabu yao na soka ya Tunisia.
Kwa barua hiyo ambayo
Tanzania Daima imebahatika kuiona nakala yake, imekuja wakati ambapo suala la
fedha hizo likianza kuhojiwa na wanachama wa klabu hiyo kwa hisia kuwa fedha
hizo zilishatoka na zimeliwa na viongozi wa klabu hiyo.
Aidha taarifa ya Etoile
du Sahel kuhusu fedha hizo, imekuja siku mbili tu tangu uongozi wa Simba utoe
taarifa kuwa bado hawajalipwa fedha za Okwi na kuwasihi wadeni wake kuvuta
subira kwani hivi karibuni watapata fedha zikiwemo hizo kutoka Tunisia.
Nyota huyo aliuzwa mapema
mwaka huu kwa kitita cha dola 300,000 za Marekani ambazo ni sawa na shilingi
mil. 450 kwa fedha za Tanzania.
Comments
Post a Comment