BUSERESERE YAIFUATA KATORO FAINALI AMANI CUP


Na Mwandishi Wetu
TIMU ya Beseresere imefanikiwa kutinga fainali ya Kombe la Amani, baada ya kuichapa Fish Star kwa mikwaju ya penalti 6-5. 
Awali, timu hizo zilikutana Jumapili iliyopita kwenye Uwanja wa CCM Katoro katika mchezo wa hatua ya nusu fainali lakini mvua kubwa iliyonyesha ikiambatana na upepo, ilisababisha mechi hiyo iahirishwe. Mpaka pambano linakatishwa, timu hizo zilikuwa sare ya mabao 2-2. 
Juzi, timu hizo zilikutana tena kwenye uwanja huo ili kutafuta mshindi atakayetinga fainali. Mpaka dakika tisini zimalizika, zilikuwa hazijafungana ambapo mara baada ya kuongezwa dakika 30 timu zote zilimaliza kwa kufungana bao 1-1. 
Buseresere ilipata bao lake kupitia kwa Adam Mathias katika dakika ya 112 kwa shuti kali huku lile la Fish likifungwa na Denis Simon katika dakika ya 114, baada ya kutokea piga nikupige katika lango la Buseresere. 
Kufuatia matokeo hayo, timu hizo ziliingia katika changamoto ya mikwaju ya penalti ambapo Buseresere iliibuka na ushindi wa penalti 6-5. 
Sasa Buseresere itaumana na Katoro katika mchezo wa fainali Jumamosi ijayo, ikitanguliwa na mchezo wa kumsaka mshindi wa tatu kati ya Ludete Star na Fish Star. 
Mratibu wa kombe hilo linalolenga kurudisha amani katika Kijiji cha Buseresere, Michael Izengo (Zagallo), alisema muitikio wa watu katika michuano hiyo ni mkubwa ambapo sasa wananchi wa kijiji hicho wamekuwa kitu kimoja tofauti na ilivyokuwa awali baada ya kutokea mauaji ya Mchungaji Mathayo Kachila, aliyeuawa kutokana na vurugu za kidini.

Comments