Mwandishi
wetu
VIONGOZI wa mataifa mbalimbali duniani, kila mara
wanakutana katika vikao vya kimataifa kusaka amani, bila amani hakuna kitu
chochote kinachoweza kufanya nchi isonge mbele.
Utasongaje mbele
wakati kila saa ni migogoro na vita? Lakini Watanzania tumejaliwa kwa kiasi
kikubwa kuwa na amani, ambayo kwa sasa kuna baadhi ya watu wanataka kuichezea. Ni
kama vile wamechoka nayo.
Lakini wakati
kukiwa na migogoro mingine ambayo haina tija, kuna kitu ambacho kimeanzishwa
ili kuwakumbusha Watanzania kuhusu misingi halisi tuliyowekewa na waasisi wa
Taifa hili.
Hiki si kingine
isipokuwa ni mbio za Uhuru Marathon, ambazo zitafanyika mwishoni mwa mwaka huu
huku Rais Jakaya Kikwete kwa kuona umuhimu wake naye ameamua kushiriki kama
kinara na jemedari wa Taifa hili ambapo mara kwa mara amekuwa akiwakumbusha
wananchi juu ya umuhimu wa kuenzi amani iliyopo..
Akithibitisha
hilo, Mratibu wa Uhuru Marathon, Innocent Melleck, anasema lengo la mbio hizo ni
kuwakumbusha Watanzania umuhimu wa kukumbuka, kuzingatia na kuuenzi urithi
waliaochiwa na viongozi waliopigania uhuru wa nchi.
Anasema urithi
huo ambao utakuwa ukikumbukwa kila mwaka kupitia mbio hizo, ni upendo,
mshikamano, umoja na amani iliyopo. Melleck anasema mbio hizo zitakuwa
zikifanyika kila mwaka na zitaanza rasmi siku ya tarehe 08/12/2013 na
zitatanguliwa na shamrashamra za kanda zote za Nchi yetu.
Hilo
lilithibitishwa pia na Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella
Mukangara , ambaye alikuwa mgeni rasmi wakati zinazinduliwa jijini Dar es
Salaam.
Uzinduzi wa mbio
hizo ulienda sambamba na kuzinduliwa rasmi kwa mtandao wa Uhuru Marathon ambao
utakuwa na habari za kila aina kuhusu mbio hizo na washirika wake.
Dk. Mukangara alipongeza wazo la kuanzishwa mbio hizo ambazo zitakuwa
zikifanyika kila mwaka, lengo likiwa ni kudumisha umoja, amani na upendo
miongoni mwa Watanzania na kuuenzi uhuru wetu.
Waziri alikiri, kwa sasa kuna mbio nyingi za marathon hapa nchini,
lakini hakuna ambaye alikuja na wazo zuri la kuanzisha mbio kama hizo za
kuuenzi uhuru wetu na kudumisha amani nchini.
“Nawapongeza waandaaji wa mbio hizi ambao ni vijana wa Kitanzania
waliokuja na wazo hili zuri la kuanzisha mbio za uhuru. Tunazo mbio nyingi sana
hapa nyumbani, lakini hatukuwa tumewaza kuanzisha mbio zinazolenga kuuenzi
uhuru wetu na kudumisha amani yetu.
“… Kwa niaba ya Serikali, napenda kusema wazi kuwa tumefurahishwa sana
na wazo hili la kuanzisha mbio hizi za Uhuru na nichukue fursa hii kuwaomba wadau
na wapenda maendeleo ya michezo kuungana na taasisi hii kufanikisha mpango huu
ili uweze kuwa na mafanikio.
“Serikali bado itaendelea kuweka miongozo na mazingira rafiki ya
kushirikiana na wadau wenye nia nzuri ya kuendeleza michezo nchini. Nina hakika
waheshimiwa mawaziri, wabunge, viongozi mbalimbali wa Serikali, mashirika
binafsi na viongozi wa dini wote watajitokeza kushiriki mbio hizi,” alisema.
Hapa ndipo
tunapoweza kusema kwamba, fikiria mbio zozote kubwa duniani kama vile London
Marathon nchini Uingereza, Paris Marathon, Ufaransa au zile zingine zenye
kupendwa na wengi zaidi duniani za Berlin Marathon zinazofanyika Ujerumani kila
mwaka, lakini Uhuru Marathon ni zaidi ya mbio.
Kwani mashindano
yote haya ni ya kutukuka, kutokana na kushirikisha wanariadha wenye majina
makubwa duniani, huku kukiwa na ushindani mkubwa zaidi miongoni mwa washiriki.
Lakini kwa sasa
Tanzania ina cha kujivunia zaidi kwa ujio wa mashindano ya mbio Uhuru Marathon.
Upekee wa
shindano hilo la Uhuru Marathon ni kutokana na aina ya washiriki wake, pamoja
na kupewa tafu kubwa na waandaaji wa mashindano ya Berlin Marathon, ambao
wanataka kuiona Tanzania inatangazwa zaidi.
Hivyo, shindano
la Uhuru Marathon, lina nafasi kubwa ya kuwabeba Watanzania kwa kutangazika
zaidi, hasa ukichukulia uzoefu mkubwa walionao waandaaji wa Berlin Marathon
ikiwa pamoja na kuchangia kudumisha amani na upendo nchini.
Mratibu wa mbio
hizo, Innocent melleck anasema, ana imani mbio hizo zitajizolea umaarufu
mkubwa, kutokana na jinsi zitakavyoteka hisia za watu mbalimbali, wakiwemo
wanamichezo.
Katika mbio hizo,
zitakazowashirikisha watu wa kada mbalimbali, zitakuwepo pia mbio za kilomita
3, kilomita 5, Half Marathon kilomita 21 pamoja na Full Marathon yenyewe
kilomita 42.
Mratibu huyo
anasema mbio za kilomita 3 zitakuwa maalumu kwa ajili ya viongozi wa kada
mbalimbali, wakiwemo pia wale wa dini na zile za kilomita 5 pia zitakuwa za
kuchangia kwa ajili ya watu wa mahitaji ya aina mbalimbali.
“Hapa tunachotaka
kufanya katika mbio za kilomita 3 ni kuwaomba kama vile viongozi maarufu wa
dini mbalimbali pamoja na viongozi wetu ili kushiriki, kwa kudumisha amani na
upendo.
“Pia
tutahakikisha kama mbio za kilomita 5, zinakuwa kwa ajili ya kuchangia watu
wenye mahitaji mbalimbali na tayari tuna uhakika mkubwa wa wanariadha maarufu
zaidi duniani kushiriki,” anasema.
Mratibu huyo
anafafanua kuwa wamejipanga mno katika hilo ili kuhakikisha wanafanya mambo
makubwa zaidi na ambayo yataleta tija kwa taifa.
Wakati Uhuru
Marathon ikitambulishwa bungeni, kiongozi aliyeonekana kufurahishwa zaidi na
hilo ni Spika Anne Makinda, ambaye hakuishia kulimwagia sifa tu, bali alitaka
hata viongozi wahakikishe wanalifanikisha.
“Ni wazo zuri
hasa katika kipindi hiki ambacho tunapigania amani na mshikamano miongoni
mwetu, tunatakiwa kuenzi mashindano kama haya ili kutufanya tuwe wamoja zaidi,”
alisema Spika Makinda.
Msaada wa Berlin Marathon
Melleck anasema,
wamefanya mazungumzo na waandaaji wa mashindano ya Berlin Marathon, kwani hilo
ni moja kati ya mashindano makubwa zaidi duniani, likiwa linashirikisha
washiriki mbalimbali walio maarufu zaidi.
Shindano la
Berlin Marathon au maarufu zaidi kwa jina la BMW Berlin Marathon kutokana na
kudhaminiwa na kampuni ya BMW ni maarufu zaidi ndani ya Ujerumani na duniani
kwa ujumla.
Shindano hilo la
Full Marathon la kiilomita 42.195 ambalo linawashirikisha wanariadha wa kulipwa
na wale wa ridhaa, lilianza kwa mara ya kwanza mwaka 1974 na linafanyika kila
wiki ya mwisho wa Septemba kila mwaka.
Shindano hili kwa
umaarufu wake, mwaka 2008 lilishirikisha wanariadha takriban 40,827 kutoka
mataifa 107, huku waliomaliza mbio wakiwa 35,913 na lina zawadi mbalimbali za
kuvutia.
Uhuru Marathon je?
Melleck anasema,
ushirikiano wa Berlin Marathon una maana kubwa, kwani itasaidia kuitangaza
zaidi Tanzania na kuifanya dunia itambue umuhimu wa amani, upendo, umoja na
mshikamano miongoni mwetu.
“Wanariadha wengi
watashiriki katika mbio hizi, wengi wakiwa maarufu zaidi duniani, pamoja na
viongozi wa kada mbalimbali na hivyo kutimiza lengo tulilojiwekea.”
Mratibu huyo
anasema, kuna kila haja kwa Watanzania, kuyathamini mashindano hayo, kwani yana
lengo la kuwafanya wawe wamoja zaidi, hasa katika kipindi hiki kigumu ambacho
kuna majaribu ya kila aina.
“Waasisi wetu wa
taifa na wale waliopigania uhuru, walikuwa na malengo mengi na tunatakiwa
kuyadumisha hayo, hilo ndilo Uhuru Marathon inalotakapigania,” anasema.
Kwa Watanzania
itakuwa faraja zaidi, hasa ukichukulia jinsi taifa linavyoweza kufaidika kwa
kuzalisha pia wanariadha wa aina mbalimbali.
Hivyo Uhuru
Marathon ni zaidi yambio, kwani inatukumbusha tulipotoka, tulipo na
tunapokwenda!
Comments
Post a Comment