(TAARIFA
KWA VYOMBO VYA HABARI)
TUZO za
Wanamichezo Bora wa Tanzania wa mwaka 2012 zinazoandaliwa na Chama cha
Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA) zitafanyika Aprili 27 mwaka huu
jijini Dar es Salaam.
Kamati
inayoratibu tuzo hiyo ilifanya kikao chake cha kwanza Jumanne wiki hii, ambapo
wajumbe wa kamati hiyo walikubaliana mambo mbalimbali ya kimsingi kuhakikisha
tuzo zinakuwa na mvuto kama ilivyokuwa miaka iliyopita na pengine ziwe bora
zaidi.
Kutokana na
hali hiyo vyama vyote vya michezo vilivyosajiliwa na Baraza la Michezo la Taifa
(BMT), ambavyo vipo hai na vinaendesha mashindano vitaandikiwa barua kwa ajili
ya kutoa mependekezo yao ya wanamichezo waliofanya vizuri kwa mwaka jana upande
wa michezo yao na yawasilishwe kabla ya Februari 28, mwaka huu.
Tunaomba
ieleweke kuwa vyama vitatoa mapendekezo na hivi sasa Kamati ya Tuzo inafanya
mazungumzo na kampuni mbalimbali zinazohusika na mambo ya mawasiliano ili kuona
namna zitakavyoshirikiana na wadau katika kuchambua majina hayo, ambapo kila
chama kimetakiwa kiwasilishe majina matano ya wanamichezo wao kwa kila jinsia
kama ni mchezo unaochezwa na jinsia mbili, lakini kama ni mchezo wa jinsia moja
watatakiwa kuwasilisha majina matano ya jinsia husika tu.
Yapo
marekebisho kadhaa yamefanyika ikiwa ni pamoja na kuongeza idadi ya tuzo kutoka
36 za mwaka jana hadi kufikia 42 mwaka huu na idadi inaweza kuongezeka ama
kupungua kulingana na sifa za wanamichezo ambazo vyama vitaleta.
Tunaomba
wadau watupe ushirikiano wa kutosha katika jambo hili ili kuzifanya tuzo ziwe
bora na kuhakikisha kila anayestahili kupata tuzo anazawadiwa kwa kuthamini
kile alichokifanya, ambapo ukumbi utakapofanyika tuzo hizo utatangazwa hivi
karibuni baada ya kukamilisha baadhi ya mambo.
Idadi ya
michezo itakayopewa tuzo pamoja na aina nyingine ya tuzo zitakazotolewa ikiwemo
Tuzo ya Heshima tutaendelea kujulishana kadri siku zitakavyokuwa zinasonga
mbele. Washindi wa kila tuzo ndiyo mmojawapo ataibuka kuwa Mwanamichezo Bora wa
Tanzania Mwaka 2012.
Dhamira ya
kamati yangu ni kutaka kuhakikisha kuwa TASWA haikukosea kututeua na tutaleta
wanammichezo sahihi na hatimaye kumpata yule bora ambaye ataungana na wengine
waliopata kutwaa tuzo hiyo miaka ya nyuma.
Wanamichezo
ambao wamepata kutwaa Tuzo ya Mwanamichezo Bora Mwaka wa Tanzania ni Samson
Ramadhan (2006), Martin Sulle (2007) na
Mary Naali (2008) wote wakiwa wanariadha, wakati mwaka 2009 alikuwa Mwanaidi
Hassan na mwaka 2010 alikuwa pia Mwanaidi Hassan ambaye ni mcheza netiboli na
mwaka 2011 alikuwa mwanasoka Shomari Kapombe.
Nawasilisha.
Haji Manara
Mwenyekiti
Kamati ya Tuzo za TASWA
01/02/2013
Comments
Post a Comment