TFF YAPONGEZA UCHAGUZI TASMA


Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linatoa pongezi kwa uongozi mpya wa Chama cha Wataalamu wa Tiba ya Michezo Tanzania (TASMA) uliochaguliwa katika uchaguzi uliofanyika Februari 10 mwaka huu jijini Dar es Salaam. 
Ushindi waliopata viongozi waliochaguliwa kuongoza chama hicho unaonesha jinsi wajumbe wa Mkutano Mkuu wa TASMA walivyo na imani kubwa kwao katika kusimamia tiba ya wanasoka nchini. 
TFF inaahidi kuendeleza ushirikiano wake kwa Kamati ya Utendaji ya TASMA chini ya uenyekiti wa Dk. Mwanandi Mwankemwa aliyeibuka mshindi katika uchaguzi huo kwa kura 18 dhidi ya 7 za aliyekuwa Mwenyekiti Biyondho Ngome. 
Uongozi huo mpya una changamoto nyingi, kubwa ikiwa ni kuhakikisha unaendesha shughuli za mpira wa miguu kwa kuzingatia katiba ya TASMA pamoja na vyombo vya mpira wa miguu vilivyo juu yake.

Pia tunatoa pongezi kwa Kamati ya Uchaguzi ya TASMA chini ya Dk. Paul Marealle na Kamati ya Uchaguzi ya TFF kwa kuhakikisha uchaguzi huo unaendeshwa kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi za Wanachama wa TFF.

Safu nzima ya uongozi wa TASMA iliyochaguliwa inaundwa na Dk. Mwanandi Mwankemwa (Mwenyekiti), Dk. Nassoro Matuzya (Katibu Mkuu), Sheky Mngazija (Katibu Msaidizi), Dk. Juma Mzimbiri (Mhazini), Joakim Mshanga (mjumbe wa Mkutano Mkuu wa TFF) na Dk. Hemed Mziray (mjumbe wa Kamati ya Utendaji).

Ukiondoa nafasi ya Mwenyekiti, wagombea wengine wote hawakuwa na wapinzani. Nafasi ya Makamu Mwenyekiti haikupata mgombea, hivyo itajazwa katika uchaguzi mdogo utakaofanyika baadaye mwaka huu.

Comments