Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linatoa pongezi
kwa uongozi mpya wa Chama cha Wataalamu wa Tiba ya Michezo Tanzania (TASMA)
uliochaguliwa katika uchaguzi uliofanyika Februari 10 mwaka huu jijini Dar es
Salaam.
Ushindi waliopata viongozi waliochaguliwa kuongoza chama
hicho unaonesha jinsi wajumbe wa Mkutano Mkuu wa TASMA walivyo na imani kubwa
kwao katika kusimamia tiba ya wanasoka nchini.
TFF inaahidi kuendeleza ushirikiano wake kwa Kamati ya
Utendaji ya TASMA chini ya uenyekiti wa Dk. Mwanandi Mwankemwa aliyeibuka
mshindi katika uchaguzi huo kwa kura 18 dhidi ya 7 za aliyekuwa Mwenyekiti
Biyondho Ngome.
Uongozi huo mpya una changamoto nyingi, kubwa ikiwa ni
kuhakikisha unaendesha shughuli za mpira wa miguu kwa kuzingatia katiba ya
TASMA pamoja na vyombo vya mpira wa miguu vilivyo juu yake.
Pia tunatoa pongezi kwa Kamati ya Uchaguzi ya TASMA chini ya
Dk. Paul Marealle na Kamati ya Uchaguzi ya TFF kwa kuhakikisha uchaguzi huo
unaendeshwa kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi za Wanachama wa TFF.
Safu nzima ya uongozi wa TASMA iliyochaguliwa inaundwa na
Dk. Mwanandi Mwankemwa (Mwenyekiti), Dk. Nassoro Matuzya (Katibu Mkuu), Sheky
Mngazija (Katibu Msaidizi), Dk. Juma Mzimbiri (Mhazini), Joakim Mshanga (mjumbe
wa Mkutano Mkuu wa TFF) na Dk. Hemed Mziray (mjumbe wa Kamati ya Utendaji).
Ukiondoa nafasi ya Mwenyekiti, wagombea wengine wote
hawakuwa na wapinzani. Nafasi ya Makamu Mwenyekiti haikupata mgombea, hivyo
itajazwa katika uchaguzi mdogo utakaofanyika baadaye mwaka huu.
Comments
Post a Comment