11/02/2013
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
KLABU ya soka ya Simba inapenda kutoa taarifa zifuatazo kwa
wadau wetu wa vyombo vya habari.
MAENDELEO YA KAMBI ARUSHA
Wachezaji wa Simba leo wameendelea na mazoezi yao mjini Arusha. Hali ya
kikosi ni nzuri . Morali ya wachezaji iko juu na hakuna mgogoro au matatizo
yoyote.
Majeruhi mpya ni mchezaji Paulo Ngalema ambaye aliumia goti
katika mechi ya juzi dhidi ya Oljoro JKT. Mchezaji huyo tayari amesafirishwa
kurejea Dar es Salaam kwa ajili ya kufanyiwa vipimo na uchunguzi zaidi.
Kutokana na tatizo hilo ,
Ngalema hataweza kucheza katika ijayo dhidi ya Libolo ya Angola katika
Ligi ya Mabingwa Afrika wikiendi ijayo.
Uongozi wa Simba unapenda kuwaarifu wapenzi na washabiki
wake kwamba hali ya timu ni shwari kabisa. Hakuna mchezaji yeyote aliyefungiwa
wala kusimamishwa na hakuna mitafuruku baina ya wachezaji na makocha au
wachezaji na viongozi wa klabu.
Washabiki walifahamu kuwa matokeo yale ya 1-1 yalikuwa ni
sehemu ya mchezo. Taarifa za kuwapo kwa vurugu zimetiwa chumvi kwa sababu
ambazo klabu yetu haizifahamu.
MECHI YA LIBOLO
TIMU ya Simba inatarajia kurejea nchini Jumatano ijayo
kutoka mjini Arusha ambako imeweka kambi ya kujiandaa na mechi dhidi ya Libolo
ya Angola .
Mechi hiyo imepangwa kufanyika Jumapili ijayo (Februari 17)
kuanzia saa kumi na nusu jioni. Uongozi unafanya utaratibu wa kuiwezesha timu
kufanya mazoezi katika Uwanja wa Taifa walau mara moja kabla ya mechi hiyo ili
kutoa nafasi kwa benchi la ufundi kutoa maelekezo mahususi kwa wachezaji
kuhusiana na mechi hiyo.
Kocha na mchezaji wa zamani wa Simba, Talib Hilal, anaelekea
Arusha leo ili kuongeza nguvu ya benchi la ufundi la Wekundu wa Msimbazi. Hii
si mara ya kwanza kwa Talib kuongeza nguvu kwenye benchi la ufundi la Simba kwani
alifanya hivyo pia miaka kumi iliyopita wakati klabu hiyo ilipocheza na Zamalek
ya Misri na kufanikiwa kuitoa.
Talib Hilal hajaja kuchukua nafasi ya mtu yeyote kwenye
benchi la ufundi. Amekuja kwa mapenzi yake kwa Simba na mara zote klabu
inamkaribisha kwa vile uwezo wake kitaaluma, uzoefu wake na uwezo wake katika
kuhamasisha unakubalika ndani ya klabu.
Unachoomba uongozi wa klabu ni uzalendo kwa taifa letu walau
katika kipindi hiki ambapo kinachoangaliwa ni utaifa wetu. Uongozi unaomba
wadau wake wa vyombo vya habari kuandika habari za kujenga umoja, mshikamano na
uzalendo kwa Watanzania wote ili hatimaye Simba ifanye vizuri.
WADHAMINI
KLABU ya Simba inakaribisha wafanyabiashara na makampuni
kujitokeza kuidhamini mechi hii kwa njia ya matangazo.
Uongozi umeamua kuuza haki za kutangaza katika Uwanja wa
Taifa itakapochezwa mechi hiyo kwa wote wanaotaka kuisaidia Simba.
Nafasi zinazouzwa ni za kutandaza mabao pembeni ya uwanja,
kutangaza kwenye televisheni kubwa iliyopo uwanjani na nje ya uwanja. Wadhamini
pia watapata fursa ya kutangazwa kupitia vyombo vya habari.
Mechi hii inasubiriwa kwa hamu na watu zaidi ya milioni 15
ndani na nje ya Tanzania .
Ni fursa ya kipekee kwa wafanyabiashara na makampuni kujitangaza.
Imetolewa na
Ezekiel Kamwaga
Ofisa Habari
Comments
Post a Comment