KIKOSI cha timu ya Taifa
‘Taifa Stars’ kimeondoka jana alasiri kwenda Addis Ababa, Ethiopia bila ya nyota wa Yanga, Kelvin Yondan na
Frank Domayo ambao walitakiwa kujiunga na timu hiyo juzi usiku wakitokea nchini
Uturuki.
Kikosi cha Stars kinakwenda
Ethiopia kwa ajili ya mchezo wa kirafiki dhidi ya wenyeji utakaopigwa kesho
katika dimba la Taifa la Addis Ababa.
Awali, Shirikisho la Soka
Tanzania (TFF) kupitia kwa Ofisa Habari wake, Boniface Wambura alisema juzi kwamba wachezaji hao wangutua nchini juzi usiku
na kuambatana na wenzao katika safari ya jana.
Akizungumza jijini Dar es
Salaam jana, kabla ya kuondoka kwenda Ethiopia, Meneja wa Stars Leopard
Mukebezi alisema kwamba wachezaji hao wataungana na wenzao Ethiopia baada ya
kushindwa kutua juzi.
Alisema mbali na wachezaji
hao, wachezaji wengineo ambao hawatakuwemo kwenye kikosi hicho ni pamoja na
Athuman Idd I ‘Chuji’ Simon Msuva na Nadir Haroub ‘Canavaro’ ambao wapo
Ututruki na klabu yao ya Yanga, Mwadini
Ally ambaye amebaki na timu yake ya Azam inayoshiriki kombe la Mapinduzi,
pamoja na John Bocco ambaye yupo nchini India kwa matibabu.
Wachezaji ambao wamekwenda
huko ni pamoja na Makipa Juma Kaseja (Simba) ambaye ndiye nahodha na Aishi Manula (Azam FC), wakati Mabeki ni
Aggrey Morris, Issa Rashid, Erasto Nyoni (Azam), Amir Maftah na Shomari Kapombe
(Simba).
Viungo ni Salum Abubakar,
Khamis Mcha (Azam), Amri Kiemba, Mwinyi Kazimoto (Simba), na Shabani Nditi
(Mtibwa Sugar).
Washambuliaji ni Mbwana
Samata, Thomas Ulimwengu (TP Mazembe, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo- DRC),
na Mrisho Ngasa (Simba).
Mchezo kati ya Stars na
Ethiopia ni maandalizi ya mwisho Ethiopia kabla ya kwenda Afrika Kusini kwenye
fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON), zitakazoanza Januari 19 mwaka
huu.
Aidha, Stars itautumia mchezo huo kama sehemu ya maandalizi
ya mechi ya mchujo dhidi ya Morocco kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Kombe
la Dunia 2014, mchezo utakaochezwa Machi mwaka huu.
Katika maandalizi yake hayo,
mara ya mwisho Stars ilicheza na Zambia ‘Chipolopolo’ Desemba 22 mwaka jana
kwenye uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam na kuibanjua bao 1-0.
Comments
Post a Comment