TIMU ya Soka ya Tanzania, Taifa
Stars leo inatarajiwa kushuka dimbani kukwaana na wenyeji wao Ethiopia bila nyota
wake Kelvin Yondani na Frank Domayo ambao wameshindwa kuungana na wenzao
wakitokea nchini Uturuki.
Nyota hao waliopo na timu yao
ya Yanga nchini Uturuki walikokwenda kwa kambi kujiandaa na
Raundi ya pili ya Ligi Kuu
Bara, walipaswa kuungana na Stars nchini Ethiopia jana, baada ya awali
kushindwa kujiunga nao jijini Dar es Salaam.
Mjumbe wa Kamati ya Utendaji
ya Yanga, Abdallah Binkleb, alisema jana kwamba, nyota hao wameshindwa kuungana
na wenzao Ethiopia, kutokana na makosa yaliyofanywa na Shirikisho la Soka
Tanzania (TFF), katika kupanga safari yao.
Alisema, nyota hao ambao
walitokea Antalya Uturuki walipopiga kambi na wenzao, walijikuta wakikwama jijini
Istanbul kutokana na kasoro hizo, hivyo uongozi wa Yanga kulazimika kuingia
gharama za kuwarejesha Antalya tena.
Awali, Yanga ilitoa ruhusa
kwa wachezaji hao wawili kati ya watano walioitwa Stars kwa ajili ya mchezo huo
huku TFF ikidai wangeungana na wenzao Ethiopia.
Mchezo wa leo ambao ni kirafiki, utakaopigwa kwenye Uwanja wa Taifa
wa Addis Ababa, ambako Stars ilitua salama Ethiopia juzi na kufikia kwenye hoteli ya Hilton.
Mechi hiyo itakayochezwa kuanzia
saa 11:30 jioni,
ni muhimu kwa timu zote kwani
wakati Ethiopia kama kipimo kuelekea fainali za Afrika, Stars inajipanga kwa
mechi ya kuwa nafasi ya fainali
za Kombe la Dunia dhidi ya
Morocco.
Fainali hizo za 29,
zimepangwa kufanyika nchini Afrika Kusini kuanzia Januari 19 hadi Februari 10, mwaka
huu.
Akizungumzia mchezo huo kabla
ya kuondoka, Kocha Mkuu wa Stars, Kim Poulsen alisema, licha
ya kuwa ni mchezo wa kirafiki,
unatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa, kwani ushindi utaongeza hamasa.
Alisema kuwa, mchezo huo pia
utakuwa na manufaa kwa Stars, kwani ni sehemu ya maandalizi ya mechi dhidi ya
Morocco, ambayo ni ya mchujo kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Kombe la
Dunia 2014, mechi itakayopigwa Machi mwaka huu.
“Nashukuru kwa kupata mechi
hii, ambayo pia itatusaidia na sisi katika maandalizi yetu dhidi ya Morocco, ni
yangu matumaini vijana watatimiza wajibu wao,” alisema.
Poulsen aliongeza kuwa,
mchezo wa leo utasaidia kumpa mwanga wa kikosi chake hicho ili kuweza
kukifanyia marekebisho pindi watakaporejea nchini.
Katika maandalizi yake hayo,
mara ya mwisho Stars ilicheza na Zambia ‘Chipolopolo’ Desemba 22 mwaka jana
kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam na kuibuka na ushindi wa mabao 1-0.
Kikosi cha Stars kinaundwa na
makipa Juma Kaseja (Simba), ambaye ndiye nahodha na Aishi Manula (Azam FC), wakati
mabeki ni Aggrey Morris, Issa Rashid, Erasto Nyoni (Azam), Amir Maftah na
Shomari Kapombe (Simba).
Viungo ni Salum Abubakar,
Khamis Mcha (Azam), Amri Kiemba, Mwinyi Kazimoto (Simba), Shabani Nditi (Mtibwa
Sugar), huku washambuliaji ni Mbwana Samata, Thomas Ulimwengu (TP Mazembe,
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo- DRC), na Mrisho Ngasa (Simba).
Comments
Post a Comment