SIMBA SC KUIVAA TIMU YA OLIMPIKI OMAN KESHO


MABINGWA wa ligi kuu soka Tanzania Bara Simba Sc, kesho watashuka katika uwanja wa Qaboos Sports Complex nchini Oman kukwaana na timu ya Taifa ya huko iliyoshiriki michuano ya Olimpiki, imefahamika.
 Simba ipo nchini Oman kwa kambi maalum ya kujiandaa na mzunguko wa pili wa ligi kuu soka Tanzania Bara  na michuano ya kimataifa.
 Katibu Mkuu wa Simba Evodius Mtawala ameiambia Sports Lady leo kwamba mchezo huo utakuwa ni muhimu kwa timu hiyo kwani kocha atautumia katika harakati zake za kukisuka ipasavyo kikosi chake. 
Kama mnavyojua tangu tumpate kocha mpya (Patrick Liewing) kikosi hajipata kukaa pamoja hivyo huo ndio mwanzo wa kocha kuanza kukiweka sawa kikosi chake,”alisema 
Mtawala aliongeza kuwa, kocha Liewing amefurahishwa na wachezaji wote kuwa pamoja kwa sasa ambapo anaamini kambi hiyo itakuwa na mafanikio zaidi. 
Mbali na mchezo huo, Simba inatarajiwa kucheza mechi nyingine za kirafiki na timu kama Fanja Fc na timu ya jeshi la huko kabla ya kurejea nchini Januari 23.

Comments