AZAM FC KULIBAKIZA KOMB E LA MAPINDUZI LEO?


                                                                        Kikosi cha Azam Fc 
Tusker Fc
FAINALI ya michuano ya kuwania Kombe la Mapinduzi inatarajiwa kupigwa leo Zanzibar kwa mabingwa watetezi, Azam FC kuwakabili mabingwa wa soka wa Kenya, Tusker katika Uwanja wa Amaan.
Wakati Azam wakikata tiketi ya fainali kwa kuing’oa Simba katika nusu fainali kwa penalti 5-4, Tusker imetoka kuitandika Miembeni mabao 2-0.
Akizungumza kwa simu kutoka Zanzibar, Kocha Msaidizi wa Azam, Kally Ongara alisema wamejipanga vizuri kutetea ubingwa wao kwa mara nyingine huku akisema mechi hiyo itakuwa ya ushindani mkubwa kutokana na umahiri wa wapinzani wao.
“Itakuwa mechi yenye ushindani mkubwa, ni mechi inayozikutanisha timu zilizofanya vizuri kuanzia hatua ya awali na ndiyo maana zikafika fainali, hivyo licha ya uwezo kila moja itakuwa ikihitaji ubingwa.
“Tumejiweka vizuri kuhakikisha kombe linabaki nyumbani kwani itakuwa aibu kombe hili liende nje ya mipaka yetu,” alisema Ongara aliyewahi kukipiga Yanga.
Azam leo itawakosa nyota wake kadhaa wakiwemo waliopo timu ya soka ya Tanzania, Taifa Stars ambayo jana ilicheza na Ethiopia mjini Addis Ababa huku nyota kama Waziri Salum, Ibrahim Mwaipopo, Abdulhalim Humud, Abdi Kassim, John Bocco, Kipre Tchetche na Jabir Aziz, wakiwa majeruhi na wengine kutumikia kadi nyekundu.
Michuano hiyo ambayo ni mahususi kwa ajili ya kuadhimisha Siku ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Januari 12, 1964, ilianza kutimua vumbi Januari 2 ikishindanisha timu za Tusker, Miembeni, Jamhuri ya Pemba, Simba, Azam FC, Coastal Union na Mtibwa Sugar.
Licha ya kila timu kujipanga kutwaa ubingwa wa michuano hiyo, filimbi ya mwisho ndio itasema kweli kama kombe litabaki kwa Azam au kutwaliwa na timu kutoka nje kwa mara ya kwanza.

Comments