LICHA ya beki Amir Maftah (Pichani) kuandika
barua ya kuomba msamaha, inadaiwa klabu yake ya Simba haina mpango tena
wakumrejesha kundini, imefahamika.
Wakati hali ikiwa hivyo kwa
Maftah, beki mwingine wa timu hiyo aliyekuwa akitumikia adhabu ya kwenda
kuongeza kiwango chake timu B, Juma Nyoso amerejeshwa kundini na jana aliungana
na wenzake katika mazoezi yanayoendelea kwenye viwanja vya TCC Chang’ombe, Temeke
jijini Dar es Salaam.
Maftah, alitakiwa kujieleza
kutokana na kushindwa kujiunga na wenzake tangu kumalizika kwa mzunguko wa
kwanza wa Ligi Kuu ya Vodacom, bila ya sababu za msingi.
Akizungumza hivi karibuni,
kiongozi mmoja wa Simba alisema, licha ya Maftah kubakiza miezi michache ya
mkataba wake, hawana mpango wa kumrejesha kundini.
Kiongozi huyo alisema kwamba,
wameamua kuachana na Maftah, kutokana na kukerwa na vitendo vyake vya utovu wa
nidhamu, ambavyo amekuwa akivifanya kwa nyakati tofauti.
Alisema, kumrejesha Maftah ni
sawa na kuruhusu kuendelea kuwepo kwa ‘virusi’ ndani ya klabu hiyo, ambavyo
vitaweza kuleta madhara makubwa katika siku za usoni.
“Simba ya sasa ni nyingine
kabisa, kwani hatuangalii majina wala uzoefu, kikubwa zaidi tunahitaji wachezaji
wenye nidhamu, kinyume na hapo huwezi kuwa na nafasi ya kuicheza Simba,” aliongeza
kiongozi huyo.
Mbali na kutojiunga na
wachezaji wenzake alipohitajiwa kwa nyakati tofauti, Maftah pia anatuhumiwa kumtukana
kiongozi mmoja wa juu wa Simba, kupitia mtandao wa kijamii wa Facebook,
akimtuhumu kumbania fedha zake za usajili.
Maftah aliyesajiliwa Simba mwaka
2011 baada ya kutemwa Yanga, mkataba wake unatarajiwa kumalizika Mei mwaka huu,
ambako kupitia barua yake hiyo ya kuomba msamaha, pia ameomba kupewa fedha zake
za usajili sh milioni nne.
Katika hatua nyingine, beki
Juma Nyoso, amerejeshwa kundini na kuungana na wenzake katika mazoezi ya
kujiandaa na mchezo wao wa ligi dhidi ya JKT Ruvu utakaopigwa Uwanja wa Taifa,
Jumapili.
Nyoso ambaye alisimamishwa
Oktoba mwaka jana pamoja na Haruna Moshi ‘Boban’, kutokana na utovu wa nidhamu
na kiwango kushuka, kabla ya uongozi kumpa adhabu ya kukichezea kikosi cha pili
cha timu hiyo.
Comments
Post a Comment