VIBAKA WASALIMISHA MALI ZA MAREHEMU SHARO MILIONEA

 Baadhi ya vitu vya marehemu Hussein Mkieti ‘Sharo Milionea’ vilivyokamatwa baada ya msako mkali uliowashirikisha Polisi na wananchi wa Kijiji Songa Kibaoni, Muheza (Picha na Bertha Mwambela,Tanga)



Mbaruku Yusuph na Bertha Mwambela, Muheza
VITU vilivyoporwa na watu wasiojuliana katika ajali ya msanii mahiri wa filamu na muziki wa kizazi kipya nchini, Marehemu Hussein Mkieti ‘Sharo Milionea’ eneo la Songa Kibaoni wilayani Muheza mkoani Tanga, vimesalimishwa na wananchi wanaosadikiwa ni wezi.
Ajali hiyo ilitokea Jumatano iliyopita eneo hilo majira ya saa 2:30 nusu usiku, baada ya gari alilokuwa akiliendesha msanii huyo, Toyota Harrier kuacha barabara na kuingia porini lilikogonga mti kisha kupinduka na kumsababishia mauti.
Msanii huyo alikuwa akitokea jijini Dar es Salaam kuelekea kijijini kwao Lusanga Muheza kwa ajili wa kuwasalimia wazazi wake pamoja na kuwapelekea fedha za matumizi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Constantine Massawe, jana alithibitisha kupatikana vitu hivyo, ambako alisema upatikanaji wake ulitokana na msako mkali uliofanywa na uongozi wa serikali Muheza wakishirikiana na Jeshi la Polisi wilayani humo.
Kamanda Massawe alisema, baada ya kutokea kwa tukio hilo, Jeshi la Polisi mkoani Tanga, liliweka mtego na kutangaza kuinunua simu ya mkononi ya msanii huyo aina ya ‘blackberry’, ndipo moja kati ya wanaodaiwa vibaka waliohusika kwenye tukio hilo, alipojitokeza na kuipeleka kwa ajili ya kuiuza.
Alisema, wakati walipofika eneo ambalo walikubaliana, walikabidhi simu hiyo kwa ajili ya kuikagua, lakini baadaye wezi hao walishtukia mtego huo na kukimbia huku wakiiacha simu hiyo.
 Aidha, Kamanda Massawe alivitaja vitu ambavyo vimesalimishwa kwa jeshi hilo kuwa ni simu ya mkononi aina ya blackberry, Betri la gari, tairi la akiba, radio ya gari, begi ambalo lilikuwa na nguo za marehemu, saa ya mkononi na nguo ambazo alikuwa amevuliwa na vibaka wa eneo hilo mara baada ya kutokea ajali hiyo.
Aliongeza kuwa, msako unaendelea na wamebaini baadhi ya washukiwa wa uhalifu huo wamezikimbia nyumba zao kwa hofu ya kukamatwa.
Alisema, hadi sasa hakuna mtu yeyote anayeshikiliwa na Polisi kuhusiana na tukio hilo la uporaji na uchunguzi wa kuwabaini waporaji ili waweze kutiwa mbaroni na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria unaendelea, huku akitoa wito kwa wananchi kuacha kufanya vitendo vya uporaji pindi ajali zinapotokea katika maeneo yao.
"Tupo kwenye uchunguzi mkali ili kuhakikisha tuwatia mbaroni wale wote ambao waliohusika na kitendo cha kinyama alichofanyiwa msanii huyo,” alisema Kamanda Massawe.
 CHANZO:GAZETI TANZANIA DAIMA

Comments