RAIS wa Shirikisho la soka Tanzania (TFF),
Leodger Tenga amewataka wachezaji wa timu hiyo kuachana na fikra ya kuwa
wapinzania wao, Congo Brazaville inaundwa na wachezaji waliozidi umri ‘Vijeba’ ,
badala yake vijana hao wajitume ili ushindi upatikane.
Hatua hiyo inafuatia kuwepo
kwa malalamiko ya Congo Brazavile kuchezesha Vijeba katika mechi yao ya awali ya kuwania
kucheza fainali za Afrika wiki iliyopita jijini Dar es Salaam ambapo Serengeti
ilishinda bao 1-0.
Tenga amesema haoni sababu ya kuwakatia rufaa kama ilivyoelezwa
awali, kwani tayari walisharipoti kwa kamishna wa mchezo huo na kama watafanya
hivyo itakuwa baadaye.
Alisema wachezaji hao hawana
budi kuelekeza akili zao kwenye mechi ya marudiano itakayopigwa ugenini
mwishoni mwa wiki hii na kuhakikisha wanashinda ili kusonga mbele.
“Nisingependa hili neno la
Vijeba liingie katika akili za hawa watoto ili waende kupambana na kurudi na
ushind,”alisema.
Aidha, Tenga amewapongeza
vijana hao kwa ushindi walioupata katika mchezo wao wa awali licha ya kuwa ni
finyu na kuwataka kuendelea na moyo wa kujituma ili waweze kufika mbali.
“Pia TFF inashukuru mashabiki
waliojitokeza kwa wingi kuja kuishangilia timu yao ,
sambamba na kamati ya kuisaidia Serengeti kwa mchango wao wa hali na mali ,”alisema.
Katika hatua nyingine, Tenga
ametolea ufafanuzi suala la mgawo wa sh mil 1 kati ya mil 23 zilizopatikana
katika mchezo wa Serengeti Boys na wenzao wa Congo Brazaville baada ya kamati
ya kuisaidia Serengeti ambayo ilichanga milioni 35 kulalamika.
Tenga alisema mil.35
zilizochangwa na kamati hiyo zilitumika kufidia hasara iliyopatikana katika
mchezo huo kwani mchezo unaofanyika katika uwanja wa Taifa na kuingiza chini ya
mil.80 ni lazima TFF ibaki na madeni.
“Ndiyo maana tumekuwa
tuklipeleka mechi bndogondogo na zile za vijana katika uwanja wa Uhuru kwa
sababu ya gharama za Uwanja wa Taifa, lakini kutokana na uwanja wa Uhuru
kutotumika ndo hatuna dudi kubaki Taifa na matokeo yake ndiyo kama
hivyo.”alisema Tenga.
Tenga aliongeza kwamba, mara
nyingi TFF imekuwa ikipata mzigo wa kulipa madeni yanayotokana na hasara za
michezo mbalimbali inayofanyika kwenye uwanja wa Taifa.
Tenga alisema kwa sasa timu
hiyo inatakiwa kuendelea kujengwa kisaikolojia ili iweze kuwa katika hali nzuri
na kufanikisha malengo yake ambayo ni muhimu kwa maendeleo ya soka la Tanzania .
Kikosi cha wachezaji 18 na
viongozi saba wa Serengeti Boys kinatarajiwa
kuondoka nchini kesho kwenda Congo Brazzavile tayari kwa mchezo huo.
Comments
Post a Comment