Juma Nyoso
MABINGWA wa soka Tanzania
Bara, Simba ya jijini Dar es Salaam inakusudia kumtoa kwa mkopo beki wake Juma
Nyoso kwa Coastal Union ya Tanga ‘Wagosi wa Kaya’, imefahamika.
Nyoso alishushwa hadi kikosi
B cha Wekundu hao wa Msimbazi kwa madai ya kushuka kiwango, sambamba na kiungo
Haruna Moshi ‘Boban’ ambaye alisimamishwa kutokana na utovu wa nidhamu kabla ya
kumalizika kwa mzunguko wa kwanza wa ligi kuu bara.
Kiongozi mmoja wa Simba
ambaye aliomba jina lake lihifadhiwe, alisema jana kwamba, wameamua kumpeleka
Nyoso Coastal kutokana na bado ana mkataba wa kuichezea Simba, lakini kama si
hivyo angekwenda na maji.
Alisema, uongozi umefikia
hatua ya kumuondoa kundini Nyoso, kutokana na ukweli kwamba, nidhamu mbovu
aliyonayo inaweza kuleta athari kwa wachezaji wengine na hasa vijana.
Kuhusiana na Boban, alisema,
suala lake bado lipo mezani kutokana na ukweli kwamba, nyota huyo ni muhimu
ndani ya klabu hiyo, lakini kasoro ndogondogo tu ndizo zinamharibia.
Alisema, tayari wachezaji hao
wamepewa barua za kujieleza kuhusiana na makosa yao na Kamati ya Utendaji ya
Simba inatarajiwa kukutana ndani ya siku mbili kwa ajili ya kutoa uamuzi rasmi juu
yao.
Comments
Post a Comment