SIMBA SC WATIMUA WANACHAMA, WAVUNJA KAMATI ZOTE

Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage akizungumza leo


KAMATI ya utendaji ya klabu ya Simba imewafuta uanachama viongozi na tawi maarufu la Mpira Pesa, sambamba na kuzivunja kamati zake ndogondogo. 
Mwenyekiti wa Simba Alhaj Ismail Aden Rage, amesema kamati ya utendaji ya Simba iliyokutana juzi ilifikia maamuzi hayo baada ya kutokea kwa chokochoko katika siku za hivi karibuni. 
Alisema mwenyekiti wa tawi hilo, Masoud Awadh na Katibu wake Ali Bane walikiuka katiba ya Simba kwa kuongea hovyo na vyombo vya habari sambamba na kuitisha mkutano wa wanachama bila ya kupata ruhusa ya uongozi. 
Rage aliongeza kuwa Awadhi si mwanachama hai wa klabu hiyo kutokana na kutolipa ada ya uanachama kwa zaidi ya miaka miwili, huku barua yake aliyouandikia uongozi  kwa niaba ya Simba nayo ni kinyume na katiba kwani hana mamlaka ya kufanya hivyo. 
Tawi la Mpira Pesa chini ya Awadhi lilifanya kikao cha kushinikiza Rage na viongozi wenzake kuachia ngazi baada ya timu kufanya vibaya katika mechi za mwisho za mzunguko wa kwanza wa ligi kuu ya Vodacom na kuishia nafasi ya tatu. 
Kama hiyo haitoshi, wanachama wa tawi hilo waliorodhesha majina zaidi ya 600 ili kutimiza akidi inayoruhusu kufanyika kwa mkutano wa dharula wa Simba. 
Hata hivyo, Rage alisema uongozi umebaini kuwa zaidi ya asilimia 90 ya wanachama waliojiorodhesha ni wafu, huku pia saini zilizowekwa ni za kughushi. 
Kuhusiana na kamati ndogondogo, Rage alisema uongozi umeona hazina msaada wowote kwa timu hivyo hivi karibuni ataunda kamati nyingine zitakazosaidia timu kupata ushindi.

Comments