Hasanoo
Na Happiness Katabazi
MWENYEKITI wa Chama cha Soka
Mkoa wa Pwani (Corefa), Hassan Othman maarufu kama Hasanoo (43) na wenzake
watano ambao wanakabiliwa na mashtaka matatu likiwemo la uhujumu uchumi na
kusafirisha pembe za ndovu zenye thamani ya sh bilioni 1.1 kwenda Hong Kong,
China katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jana aliwasilisha ombi la kuomba
dhamana na Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.
Hassanoo ambaye anatetewa na
wakili wa kujigetemea Richard Rweyongeza, ndiye aliyewasilisha maombi hayo kwa njia
ya maandishi kwa niaba ya mshtakiwa huyo anayesota gerezani tangu alipofikishwa
katika mahakama ya Kisutu Ijumaa iliyopita akikabiliwa na kesi hiyo mpya ya
kusafirisha pembe za ndovu.
Wakili Rweyongeza, alifikia
hatua ya kuwasilisha ombi hilo
jana kutokana na mahakama ya Kisutu kutokuwa na mamlaka ya kusikiliza kesi
hiyo, pia Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP),
Dk. Eliezer Feleshi, hakutoa kibali cha kuruhusu kesi hiyo isikilizwe katika
Mahakama ya Kisutu.
Novemba 23 mwaka huu, siku
ambayo kesi hii ilifunguliwa, Wakili Mwandamizi wa Serikali, Shedrack Kimaro mbele ya Hakimu
Mkazi Augustina Mbando, alidai kuwa mbali na Hassanoo, washtakiwa wengine ni
Ally Kimwaga, Dastan Mwanga, Godfrey Mwanga, John Mlay na Khalid Fazaldin.
Kimaro alidai, shtaka la
kwanza ni la kula njama na kujihusisha na biashara haramu ya kusafirisha nyara
za serikali bila leseni ambalo walilitenda
kati ya Septemba Mosi na Novemba 20, mwaka huu, Dar
es Salaam na Hong Kong kinyume na
kifungu cha 384 cha Sheria ya Kanuni ya
Adhabu ya mwaka 2002.
Katika shitaka la pili, washtakiwa
hao kwa nia ovu walipanga, wakatekeleza, wakasimamia na kuwezesha kifedha kufanyika kwa biashara hiyo haramu ya
kutorosha vipande 569 vya pembe za ndovu, vyenye uzito wa kilo 1330 na thamani
ya sh 1,185,030,000 kwenda Hong Kong, kosa ambalo walilitenda kati ya Septemba
Mosi na Novemba 20 mwaka huu, kusafirisha nyaraka hizo kutoka Dar es Salaam
kwenda Hong Kong.
Aidha, alidai shtaka la tatu
kuwa, siku hiyo ya tukio, washtakiwa walijihusisha na biashara hiyo ya nyara za
serikali kinyume na kifungu cha 80 na 34
ya uhifadhi wa Wanyama Pori namba 5.
Aliongeza kwa kudai kuwa,
washtakiwa hao kwa nia ovu waliendesha biashara hiyo ya nyara za serikali bila
ya kuwa na kibali halali kinachowaruhusu kufanya biashara hiyo.
Mbali ya kesi hiyo, Hasanoo
aliyewahi kuwa Katibu wa Klabu ya Simba, pia anakabiliwa na kesi nyingine ya
wizi wa tani 26.475 za madini aina ya Shaba
zenye thamani ya sh 333,
467,848.13 kutoka Zambia
kinyume na kifungu cha 258, 265 na 269 (c) vya kanuni ya adhabu, mali
ya Kampuni ya Liberty Express Tanzania Ltd ambayo ilifunguliwa mahakamani hapo
mwaka jana na imefikia hatua ya kuanza kusikilizwa.
Comments
Post a Comment