AZAM JUU YA SIMBA LIGI KUU

Kipre Tcheche


Na Prince Akbar, Chamazi
AZAM FC imezunduka tena baada ya kuichapa JKT Oljoro 1-0 kwenye Uwanja wake wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam katika mfululizo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara jioni hii.
Shujaa wa Azam leo alikuwa ni mshambuliaji wa Ivory Coast, Kipre Herman Tcheche aliyefunga bao hilo pekee dakika ya nne kwa mkwaju wa penalti, baada ya Yassin Juma kuunawa mpira kwenye eneo la hatari. Katika mchezo huo, Azam ilimpoteza kiungo wake Himid Mao dakika ya 88 aliyelimwa kadi nyekundu kwa kucheza rafu.
Ushindi huo, unaifanya Azam ifikishe pointi 24 baada ya kucheza mechi 12 na sasa inapanda hadi nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu, ikiizidi Simba kwa pointi moja, ambayo pia imecheza mechi 12. Yanga yenye pointi 26, inaendelea kuongoza ligi hiyo baada ya kucheza mechi 12 pia.
Katika mechi nyingine za ligi hiyo, bao pekee la Daniel Lyanga dakika ya tatu, limeipa ushindi wa 1-0 Coastal Union dhidi ya Polisi Moro Uwanja wa Mkwakwani, Tanga, wakati bao pekee la beki Issa Rashid dakika ya 26 limeipa Mtibwa Sugar ushindi wa 1-0 dhidi ya JKT Ruvu, Uwanja wa Manungu, Turiani Morogoro.
Ligi hiyo inatarajiwa kuendelea Jumamosi, Simba na Toto African Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Mgambo JKT na Azam FC Uwanja wa Mkwakwani, Tanga, African Lyon na Mtibwa Sugar Chamazi, Dar es Salaam, Prisons na JKT Ruvu Sokoine, Mbeya, Kagera Sugar na Polisi Morogoro, Kaitaba, Bukoba na JKT Oljoro na Ruvu Shooting Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha.
Mchezo wa kukamilisha mechi za mzunguko wa kwanza utachezwa Uwanja wa Mkwakwani, Tanga Jumapili kati ya Yanga na Coastal Union.

Comments