YANGA NYUMA KABISA YA SIMBA NA AZAM


Jerry Tegete akimtoka beki wa Ruvu Shooting jana. Picha na habari kutoka bongostaz.blogspot.com
 YANGA SC jana imetoka nyuma kwa mabao 2-0 na kushinda 3-2 dhidi ya Ruvu Shooting katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara uliofanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Ushindi huo, unaifanya Yanga itemize pointi 14, baada ya kucheza mechi nane, hivyo kujiweka sawa katika nafasi ya tatu, ikizidwa pointi tatu na Azam inayoshika nafasi ya pili na pointi nne na Simba inayoongoza ligi hiyo.
Hadi mapumziko timu hizo zilikuwa zimekwishafungana mabao 2-2, Ruvu Shooting wakitangulia na baadaye Yanga kusawazisha.
Mabao ya Ruvu yalifungwa na mshambuliaji Seif Abdallah dakika ya tatu na lingine dakika ya 10, yote kutokana na mipira kutoka upande wa kulia mwa Uwanja, la kwanza mpira wa adhabu na la pili krosi.
Ruvu, inayofundishwa na kocha na mchezaji wa zamani wa Yanga, walitumia mwanya wa beki wa kulia wa Yanga, Oscar Joshua kutopata msaada wa viungo wa timu hiyo anapopanda kusaidia mashambulizi.
Baada ya bao la pili, kocha Mholanzi, Ernie Brandts alimuinua Juma Seif ‘Kijiko’ akitaka kufanya mabadiliko ya safu ya kiungo iliyokuwa inaundwa na Nurdin Bakari upande wa ulinzi na Rashid Gumbo upande wa mashambulizi, lakini hakufanya hivyo hadi kipindi cha pili.
Lakini haikuchukua muda mrefu wakati Kijiko ‘anatroti’ safu ya kiungo ya Yanga iliyokuwa inaboronga ikaanza kucheza vizuri na kusaidia timu hiyo kurudisha mabao hayo.
Rashid Gumbo aliangushwa nje kidogo ya eneo la hatari na Mbuyu Twite akaenda kupiga mpira wa adhabu uliotinga moja kwa moja nyavuni dakika ya 20 na haraka haraka Jerry Tegete akauchukua mpira kwenye nyavu za Ruvu na kwenda kuuweka katikati.
Hilo lilikuwa bao la pili Twite anaifungia Yanga kwenye ligi, ndani ya mechi nane alizocheza.
Krosi nzuri ya beki wa kulia, Juma Abdul iliunganishwa vema kimiani na Tegete dakika ya 36 na kuifanya Yanga iwe sawa na Ruvu. Kutoka hapo, Yanga waliuteka zaidi mchezo na walikaribia kufunga bao la tatu dakika ya 40, kama pasi nzuri ya Didier Kavumbangu ingeunganishwa vema kimiani na Gumbo.
Kipindi cha pili Yanga walirudi na kasi tena na kufanikiwa kupata bao la ushindi dakika ya 65, ambalo lilifungwa na Kavumbangu, baada ya kutokea kizazaa langoni mwa Ruvu.
Baada ya bao hilo, Ruvu walizinduka nao kuanza kujibu kwa mashambulizi langoni mwa Yanga na walikaribia kufunga mara mbili, mara moja kipa Yawe Berko akiokoa na mara moja shuti la Seif Abdallah kugonga mwamba wa juu ya lango na kurudi uwanjani, kabla ya Oscar Joshua kuondosha kwenye eneo la hatari.
Baada ya mchezo huo, kocha wa Ruvu, Charles Boniface Mkwasa pamoja na kujutia nafasi walizopoteza, lakini aliwalalamikia marefa wa mechi hiyo kwa kuwapendelea Yanga, wakati kocha wa wapinzani wake, Mholanzi Ernie Brandts alisema hawakuanza vizuri, lakini walitulia na kucheza vizuri, hatimaye wakashinda- hivyo kuwapongeza vijana wake kwa kazi nzuri.
Katika mchezo huo, kikosi cha Yanga kilikuwa; Yanga SC; Yaw Berko, Juma Abdul/Juma Seif, Oscar Joshua, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Mbuyu Twite, Rashid Gumbo/Shamte Ally, Nurdin Bazkari, Haruna Niyonzima, Jerry Tegete/Hamisi Kiiza, Didier Kavumbangu na David Luhende.
Ruvu Shooting; Benjamin Haule, Michael Aidan, Baraka Jaffari, George Assey/Mangasini Mbonosi, Ibrahim Shaaban, Ernest Ernest, Raphael Kyala/Ayoub Katala, Hassan Dilunga, Seif Abdallah, Abrahman Mussa na Said Dilunga/Kulwa Mobi.
Katika mchezo mwingine wa ligi hiyo kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Tanga, Coastal Union iliifunga Mtibwa Sugar mabao 3-1 mabao ya Juma Jabu, Daniel Lyanga na Lameck Dayton, la Mtibwa lilifungwa na Shaaban Nditi.

Comments