PAMBANO LA SIMBA, OLJORO JKT LAINGIZA MIL 46/-


Pambano la Ligi Kuu ya Vodacom kati ya Simba na Oljoro JKT ya Arusha lililochezwa jana (Oktoba 7 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kumalizika kwa wenyeji kuibuka na ushindi wa mabao 4-1 limeingiza sh. 46,680,000.
 
Watazamaji 8,081 walikata tiketi kushuhudia mechi hiyo kwa viingilio vya sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh. 20,000 huku kila klabu ikipata mgawo wa sh. 8,172,396.61 wakati Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) iliyolipwa ni sh. 7,120,677.97.
 
Mgawo mwingine wa mapato hayo ni posho ya msimamizi wa kituo sh. 120,000, kamishna wa mechi sh. 193,000, waamuzi sh. 210,000, mwamuzi wa akiba (reserve referee) sh. 70,000, usafi na ulinzi wa uwanja sh. 2,350,000 na Wachina (stadium technical support) sh. 2,000,000.
 
Umeme sh. 300,000, maandalizi ya uwanja (pitch preparation) sh. 400,000, ulinzi wa mechi sh. 3,500,000 wakati tiketi ni sh. 3,175,000. Gharama za mchezo sh. 2,724,132.20, uwanja sh. 2,724,132.20, Kamati ya Ligi sh. 2,724,132.20, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 1,634,479.32 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 1,089,652.88.
 
PONGEZI KWA UONGOZI MPYA ARFA
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linatoa pongezi kwa uongozi mpya wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Arusha (KRFA) uliochaguliwa katika uchaguzi uliofanyika jana (Oktoba 7 mwaka huu).
 
Ushindi waliopata viongozi waliochaguliwa kuongoza chama hicho unaonesha jinsi wajumbe wa Mkutano Mkuu wa ARFA walivyo na imani kubwa kwao katika kusimamia mchezo huo mkoani Kigoma.
 
TFF inaahidi kuendeleza ushirikiano wake kwa Kamati ya Utendaji ya ARFA chini ya uenyekiti wa Khalifa Mgonja ambaye amechaguliwa tena kuongoza chama hicho.
 
Uongozi huo mpya una changamoto nyingi, kubwa ikiwa ni kuhakikisha unaendesha shughuli za mpira wa miguu mkoani Arusha kwa kuzingatia katiba ya ARFA pamoja na vyombo vya mpira wa miguu vilivyo juu yake.
 
Pia tunatoa pongezi kwa Kamati ya Uchaguzi ya ARFA na Kamati ya Uchaguzi ya TFF kwa kuhakikisha uchaguzi huo unaendeshwa kwa mujibu wa kanuni za uchaguzi za wanachama wa TFF.
 
Viongozi waliochaguliwa katika uchaguzi huo ni Khalifa Mgonja (Mwenyekiti), Seif Banka (Makamu Mwenyekiti), Adam Brown (Katibu), Peter Temu (Mjumbe wa Mkutano Mkuu TFF), Omari Walii (Mwakilishi wa Klabu TFF) na Mwalizo Nassoro (Mhazini).
 
Waliochaguliwa kuwa Wajumbe wa Kamati ya Utendaji katika uchaguzi huo uliofanyika Leganga, Usa River ni Hamisi Issa, Athuman Mhando na Eliwanga Mjema. Nafasi ya Katibu Msaidizi iko wazi na itajazwa katika uchaguzi mdogo utakayofanyika baadaye.
 
Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

Comments