MMOMONYOKO WA MAADILI KATIKA SEKTA YA SANAA.


Kutokana na kushuhudiwa kwa mmomoyoko wa maadili katika sekta ya sanaa katika siku za hivi karibuni, Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA), limeandaa  kongamano la pamoja la wadau kujadili juu ya hali hiyo ili kupata mapendekezo ya nini kifanyike na hatua gani zichukuliwe kukabiliana na hali hiyo. 
Katibu Mtendaji wa BASATA, Ghonche Materego, amesema kongamano hilo litafanyika Jumatatu ya terehe 15/10/2012 katika Jukwaa la Sanaa kuanzia saa 4:30 asubuhi ambapo mada itakuwa ni ‘Mchango wa vyombo vya habari katika kudhibiti au kuchochea mmomonyoko wa maadili katika sekta ya sanaa’. 
Ghonche amewakaribisha wadau wote ili kuleta michango, mapendekezo na hoja mbalimbali katika kuleta mustakabali utakaojenga sekta ya sanaa yenye maadili na itakayokuwa na tija kwa utamaduni wa taifa. 
Amesema kongamano hilo litaongozwa na Mkuu wa Shule Kuu ya Uandishi wa Habari na Mawasiliano ya Umma ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (SJMC) Dkt. Herbet Makoye  ambaye atakuwa Mwenyekiti, na wajumbe wazungumzaji watakuwa ni Bishop Hiluka (mwandishi na mtunzi), Harrieth Makweta (mwandishi) Khadija Khalili (mwandishi), Wilson Makubi (Katibu Shirikisho la Filamu) Ado Novemba ambaye ni Rais wa Shirikisho la Muziki na  Edna Rajabu (TBC).
 
Hatua hiyo ya BASATA imekuja wiki moja baada ya kutoa maelekezo kwa mashirikisho ya sanaa kushughulikia suala la mmomonyoko wa maadili na kuwachukulia hatua wasanii wanaohusika na vitendo vya kujidhalilisha na kuidhalilisha tasnia ya sanaa na jamii kwa kuwa nusu utupu au kuandaa sanaa zinazokiuka maadili.

Comments