LIGI DARAJA LA KWANZA KUANZA OKT.20


Kamati ya Ligi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) ilikutana jana (Oktoba 5 mwaka huu) kupitia na kufanya uamuzi katika masuala mbalimbali na kupanga Ligi Daraja la Kwanza (FDL) ianze kutimua vumbi Oktoba 20 mwaka huu. 
Timu zimepangwa katika makundi matatu ya timu nane nane ambapo zitacheza ligi hiyo kwa mtindo wa nyumbani na ugenini. Mshindi wa kila kundi ndiye atakayepata tiketi ya kucheza Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) msimu ujao wakati timu ya mwisho kila kundi itashuka daraja kurudi Ligi ya Mkoa. 
Kundi A lina timu za Burkina Moro ya Morogoro, Kurugenzi Mufindi ya Iringa, Majimaji ya Songea, Mbeya City ya Mbeya, Mlale JKT ya Ruvuma, Mkamba Rangers ya Morogoro, Polisi Iringa na Small Kids ya Rukwa.

Ndanda FC ya Mtwara, Ashanti United, Green Warriors, Moro United, Polisi, Tessema, Transit Camp na Villa Squad zote za Dar es Salaam ndizo zinazounda kundi B wakati kundi C ni Kanembwa JKT ya Kigoma, Morani ya Manyara, Mwadui ya Shinyanga, Pamba ya Mwanza Polisi Dodoma, Polisi Mara, Polisi Tabora na Rhino Rangers ya Tabora.

Ada ya ushiriki wa ligi ni sh. 200,000 zinazotakiwa kulipwa kabla ya Oktoba 13 mwaka huu. Pia Oktoba 13 mwaka huu kutakuwa na kikao kati ya wenyeviti wa klabu zote zinazoshiriki ligi hiyo na Kamati ya Ligi ambapo pia itafanyika draw (ratiba).

Comments