VODACOM YAWATOA WASIWASI WADAU WA SOKA KUHUSINA NA UDHAMINI WA LIGI KUU BARA

Dar es Salaam, 30 Septemba, 2012. Kufuatia kukaa katika kikao cha majadiliano kati ya Mdhamini mkuu wa ligi kuu Vodacom Tanzania, kamati ya ligi, TFF na vilabu vinavyoshiriki ligi hiyo, Mashabiki na wapenzi wa soka nchini wameondolewa hofu juu ya udhamini wa ligi inayoendelea hivi sasa.
Mdhamini mkuu wa ligi hiyo Vodacom Tanzania, imekubali kuendelea kuunga mkono ligi hiyo na kuwaomba mashabiki wa soka kutegemea msimu mzuri wa ligi mwaka huu.
Kwa mujibu wa Mkuu wa Kitengo cha Masoko na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania, Kelvin Twissa, amesema kuwa mvutano ambao umekuwepo baina ya baadhi ya Vilabu vya soka na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) pamoja na wadhamini sasa yamepatiwa ufumbuzi.
“Kulikuwa na sinto fahamu kati ya Klabu za ligi kuu TFF na sisi kama wadhamini, tulikaa kikao siku ya ijumaa na wadau wote wa ligi na sasa mambo yote yamewekwa katika msitari,” alisema Kelvin na kuongeza kuwa “ Tumedhamiria kuendelea kuiunga mkono Ligi kuu ya Vodacom hatukuwa na matatizo yoyote katika kusaini mkataba na kamati ya ligi ni ufafanuzi tu ndio ulihitajika  ili kuwekana sawa,” alisema Twissa.
Kuhusiana na kutolewa kwa fedha za udhamini na uendeshaji wa ligi na udhamini wa kampuni pinzania twissa alisema Vodacom haizuii klabu za ligi kudhaminiwa na kampuni nyingine yoyote tofauti na zile zenye msingi wa kiushindani katika biashara na kampuni hiyo.
“Kufuatia kikao hicho na kuwa katika msitari mmoja tumekwisha toa fedha na vifaa kwa TFF na vilabu ili ligi iweze kwenda kama ilivyo takiwa,Tukiwa kama wadau katika kuunga mkono maendeleo ya soka nchini, tumeruhusu kampuni nyingine ambazo hazina upinzani wa kibiashara na sisi ili kuondoa muingiliano wa kimaslahi,” alisema.
“TFF inadhamana ya kusimamia sheria na masharti kuhusu ligi. Hatuna matatizo yoyote ya kiutendaji na TFF wala klabu yoyote” alihitimisha Twissa.
Ligi kuu ya Vodacom ilianza rasmi tarehe 15  mwezi septemba, na tutashuhudia michezo 182 kwa kushirikisha timu 14 zinazoshiriki katika ligi hiyo, zikiwemo Yanga Afrika, Kagera sugar, na Simba ambaye ndie bingwa mtetezi wa ligi kuu ya Vodacom.
Kampuni ya Vodacom imekuwa mdhamini wa ligi kuu kwa miaka mitano sasa, na imesaini mkataba mpya wa udhamini wa ligi hiyo kwa miaka mitatu na shirikisho la mpira wa miguu TFF, mkataba utakao shuhudia shirikisho hilo likipokea udhamini wa kila msimu kwa miaka mitatu mfululizo.
 

Comments