VODACOM TANZANIA YASAINI MKATABA WA KUDHAMINI LIGI KUU BARA


 Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom,Rene Meza akimfafanulia jinsi mkataba ulivyo wa udhamini wa ligi kuu ya Vodacom Tanzania bara Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Ligi ,Said Mohamee,katika hafla iliyofanyika jijini Dar es Salaam,wanaoshuhudia wapili toka kushoto Makamu wa kwanza wa Rais wa TFF,  Athuman Nyamlani,Ofisa Mkuu wa maswala ya  Sheria wa Vodacom Bw.Wallarick Nittu.
Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom,Rene Meza akimkabidhi Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Ligi , Mohammed Said mkataba wa udhimini wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania bara,katika hafla iliyofanyika jijini Dar es Salaam.


Dar es Salaam, 11 Septemba, 2012……. Shirikisho la mpira wa miguu Tanzania (TFF) leo limeingia katika mkataba wa udhamini kutoka kwa kampuni ya mawasiliano ya Vodacom Tanzania, wakati maandalizi ya ligi kuu ya Vodacom Tanzania yakielekea ukingoni.
Kampuni ya Vodacom imekuwa mdhamini wa ligi kuu kwa miaka mitano iliyopita, na sasa imeingia mkataba mpya wa udhamini kwa miaka mitatu na TFF, mkataba utakao liwezesha shirikisho hilo kupoea fedha za udhamini kwa miaka mitatu.
Ligi kuu ya Vodacom itaanza tarehe 15 ya mwezi huu, ikitarajia kushuhudia michezo 182 ikichezwa katika viwanja mbalimbali na kushirikisha timu 14, zikiwemo timu za Dar es Salaam Young Africans, Kagera Sugar na  Simba Sports Club ambaye ndie bingwa mtetetzi wa kombe hilo.
Mkurugenzi mtendaji wa Vodacom Tanzania, Rene Meza, amesema kuwa kampuni ya Vodacom iko katika mstari wa mbele katika kuunga mkono maendeleo na shughuli mbalimbali za kimichezo ndani ya nchi. 
“Wanamichezo wote ni mabalozi wazuri katika nchi. Ni wajibu wetu kuhakikisha kuwa tunawaunga mkono katika kutambua na kukuza vipaji vyao kadri tutakavyo weza,” alisema Meza na kuongeza kuwa, “Kama jina linavyojulikana ligi kuu ya Vodacom, kombe hili linashuhudiwa na mashabiki zaidi ya milioni 10 katika mechi 182 zitakazo chezwa sehemu mbalimbali za Tanzania bara.”
Meza amejivunia kampuni hiyo kuwa wadhmini wa ligi kuu kwa kipindi kingine, na kufafanua kuwa mpira wa miguu ndio unaongoza kitaifa na unapendwa na Watanzania wengi.
Michuano ya mwaka huu itashuhudia timu mpya tatu ambazo ni timu ya Polisi Morogoro, Tanzania Prisons na Mgambo JKT. Mkataba huu umehusisha pande zote ambazo ni kampuni ya Vodacom Tanzania, Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na kamati ya ligi.
Kwa upande wake makamu wa Rais wa TFF, Nasibu Nyamlani, ameipongeza kampuni ya Vodacom Tanzania akisema kuwa anaamini kuwa maendeleo ya sasa yatalenga zaidi katika kuunga mkono vipaji vipya na vilivyopo ndani ya nchi.
“Kwa niaba ya TFF, napenda kuwashukuru Vodacom Tanzania kwa kuonyesha nia na kuendelea kuunga mkono mpira wa miguu nchini. Nasi tunaahidi kuendelea kuthamini vipaji vya wachezaji wetu na kuhakikisha tunapata mafanikio zaidi,” alisema Nyamlani.

Comments