YANGA KWENDA KUJINOA RWANDA


MABINGWA wa soka Afrika Mashariki na Kati, Yanga ya jijini Dar es Salaam, wanatarajiwa kufanya ziara maalumu ya kimchezo nchini Rwanda, imefahamika.
Habari za kuaminika kutoka ndani ya klabu hiyo yenye maskani yake mitaa ya Jangwani na Twiga, zinaeleza kwamba, kutokana na muda kuwa mfupi kabla ya kuanza kwa Ligi Kuu Tanzania Bara, wameona ni bora kwenda nchini humo kujinoa.
Kiongozi mmoja wa Kamati ya Utendaji ya Yanga, alimweleza Mwandishi wa Habari hizi kwamba, awali kulikuwa na mipango ya kuipeleka kambini katika moja ya nchi barani Ulaya, lakini kutokana na muda kutoruhusu wameona waipeleke Rwanda.
Alisema tayari wamefanya mazungumzo na Shirikisho la Soka nchini humo (FERWAFA), kuhusiana na ziara hiyo, ambapo wako katika hatua nzuri na wiki ijayo itatolewa taarifa rasmi juu ya hilo.
Aliongeza kuwa ikiwa huko, Yanga inatarajiwa kucheza na timu za Atraco, Polisi Rwanda, Rayon na APR.
Yanga kwa sasa inaendelea na mazoezi yake ya kujiandaa na michezo mbalimbali, ikiwemo Ligi Kuu Tanzania Bara inayotarajiwa kuanza Septemba mosi mwaka huu.

Comments