WAREMBO MISS TANZANIA KUJENGA MABWENI


Miss Tanzania 2005 Nancy Sumari (kushoto) na Miss Tanzania namba mbili 2005 Jokate Mwegelo (kulia) na washirika wenzao katika mpango huo Maryam Ndaba na Rebecca Gyumi

Kikundi cha wasichana maarufu watano katika nyanja mbalimbali nchini wameungana kwa pamoja na kuamua kwa hiari kuunga mkono jitihada za Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) za kutafuta kiasi cha shilingi za kitanzania billion 2.3 zitakazotumika kujenga hosteli 30 ambazo zitahudumia wasichana wa shule za sekondari 1,504.

Kikundi hicho cha mabalozi wa kampeni hii kinaundwa na Rebeca Gyumi(Mtangazaji wa kipindi cha FEMA) Faraja Nyalandu (Miss Tanzania 2004), Nancy Sumari (Miss Tanzania 2005) Jokate Mwegelo(Mshindi wa pili Miss Tanzania 2006) na Mariam Ndaba(Mwana mitindo na mmiliki wa blog) kiliguswa kwa namna ya kipekee na na jitihada za TEA na hivyo wakaamua kwa hiari kuungana na TEA katika kuhamasisha watu kujitokeza na kuchangia kampeni hii.

Mabalozi hawa wameiita kampeni yao “Elimu Yao. Wajibu wetu” maana ya usemi huu ni kwa kila mtanzania ana wajibu wa kuhakikisha mtoto wa kike anapewa haki yake ya kuwa na elimu bora. Haki hii ya elimu inajumuisha mazingira mazuri ya kusomea. Hivyo huu ni wito kwa watanzania, wafanyabiashara, wafanyakazi, wanawake watanzania waliofanikiwa na watanzania wa ughaibuni kujitokeza kwa wingi na kuhusika moja kwa moja na jitihada hizi.
Changamoto ambazo mtoto wa kike anakumbana nazo hususani anayetokea nyumbani kwenda shule ni pamoja na kukosa muda wa kujisomea kutokana na kazi za nyumbani ambazo zinapelekea kuathiri maendeleo ya elimu kwa mtoto wa kike, mimba na ndoa za utotoni ni kati ya changamoto kubwa zinazowakumba wale waliopanga karibu na maeneo ya shule, kutokana na hayo, Mabalozi hawa wameamua kujitolea kwa kuweka mpango mkakati utakaosaidia ujenzi wa hosteli tano na kuendelea kati ya hizo 30 ambao TEA imepanga kujenga.

Mpango mkakati huo ni pamoja na kufanya kampeni katika vyomba mbalimbali vya habari nchini na kuandaa  mbio za hisani ambapo hela zitakazopatikana zitapelekwa katika mradi huo. Mabalozi hawa wanaamini kuwa tofali moja kutoka kwa kila mtanzania linaweza kuleta mabadiliko “changia Tofali”. Unaweza kuchangia kwa kutuma neno "Changia Tofali"kwenda namba 15564, na utakuwa umechangia Tshs 250/-. Changia mara nyingi uwezavyo.
Tunakuomba mchango wako wewe mzazi, wadau wa elimu na watanzania kwa ujumla wenu kuchangia katika kampeni hii. Mchango unaweza kuwa ni wa fedha taslimu au vifaa vya ujenzi wa hosteli na samani. Kwa upande wa fedha taslimu unaweza kuweka fedha katika akaunti ya “mfuko wa elimu” benki ya CRDB, namba ya akaunti 01J027639900 au kupitia akaunti ya M-pesa 404040, au tuma ujumbe Changia Tofali kwenda namba 15564. Pia unaweza kuleta mchango wako katika ofisi zetu zilizopo mikocheni barabara ya kambarage au kupitia vituo vya Televisheni vya ITV, Channel 10 na Star TV.

Comments