SUALA LA YONDAN, REDONDO KUAMULIWA NA MGONGOLWA


WAKATI timu zote za Ligi Kuu Bara zikiwasilisha usajili wao, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), limesema Kamati yake ya Sheria, Katiba na Haki za Wachezaji chini ya Mwenyekiti wake Alex Mgongolwa, ndiyo itakayotoa uamuzi juu ya utata wa wachezaji Ramadhan Chombo ‘Redondo’ na Kelvin Yondan.
Hatua hiyo inatokana na majina ya wachezaji hao kupelekwa na timu mbili tofauti ambako Redondo aliyekuwa akiichezea Azam msimu uliyopita, jina lake limeorodheshwa pia na Simba huku Yondani aliyekuwa kwa Wekundu wa Msimbazi ameorodheshwa kwenye kikosi cha Yanga.
Akizungumza na Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam jana, Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah, alisema kamati hiyo inatarajiwa kuketi Agosti 23 na 24 kupitia usajili wa wachezaji wa klabu za Ligi Kuu Bara na Ligi Daraja la Kwanza, ambako zoezi hilo lilifungwa
juzi saa sita usiku.
Alisema, kuhusiana na Yondani, Simba imewasilisha mkataba wake tu bila ya kuwemo kwenye fomu mama ya klabu hiyo, huku Redondo jina likishindwa kuorodheshwa katika fomu mama ya Azam Fc na pia kukosekana baadhi ya vielelezo, pamoja na mkataba wake ambao unaishia Juni mwakani.
Osiah aliongeza kuwa, ukiachana na hilo, timu zote 14 zitakazoshiriki ligi hiyo itakayoanza Septemba Mosi mwaka huu, ziliwasilisha fomu huku Toto African ya Mwanza ikiwa ya mwisho kufanya hivyo, baada ya kupata tabu katika kusajili kwa njia ya kompyuta kabla ya TFF kuipa ushirikiano.
Alisema, kwa upande wa timu za daraja la kwanza ni timu tano tu kati ya 24 zilizowasilisha usajili wake na kuwa, huenda hali hiyo inatokana na mchakato wa kusajili kwa kompyuta kuwatatiza wengi.
Aliongeza kuwa, kutokana na hali hiyo, wameiagiza Kamati ya Mgongolwa, kukutana haraka ili kuangalia jinsi ya kufanya kwani kanuni zipo kimya juu ya hilo.
Osiah alizitaja timu za Daraja la Kwanza zilizowasilisha usajili ni Polisi Dar Central, Taseme, Mkamba Rangers Fc, Transit Camp na Moro United.

Comments