SIMBA, AZAM FC LEO KATIKA NUSU FAINALI YA BANC ABC SUP8R CUP



NUSU fainali ya michuano ya BancABC SUP8R inatarajiwa kutimua vumbi leo kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam kwa mechi mbili kupigwa kwenye dimba hilo.
Simba watashuka dimbanikuwakabili Wanalambalamba Azam FC huku mechi ya kwanza ikichezwa mapema kuanzia saa 8:00 kati ya Jamhuri ya Pemba na Mtibwa Sugar.
Ofisa habari wa Simba alisema wamejipanga vya kutosha na ana imani vijana wake  watapigana kufa  au kupona ili kulileta kombe hilo Msimbazi, maana ni kama kawaida yao  michuano yoyote inapoanza, kubeba ubingwa. "Hii BancABC SUP8R, ni ya kwanza, kwa hiyo kombe ni la Msimbazi japokuwa lolote linaweza tokea,” alisema Kamwaga.
Naye Kocha Mkuu wa Jamhuri, Amiry Chuwa, alisema wao leo watapambana kuhakikisha wanashinda ili kutinga fainali, kutokana na maandalizi waliyofanya tangu kuanza kwa michuano hiyo.
Naye Kocha wa Mtibwa Sugar, Mecky Mexime, alisema  wanajiamini katika mchezo huo kutokana na kiwango chao huku akiwataka wadhamini BancABC SUP8R, kutokata tamaa kwa kuwa soka la bongo lina zengwe.
“Soka la bongo ni zengwe tupu, hivyo nyie wadhamini nawashauri msikate tamaa, muhimu muwe na mioyo migumu msitishwe na zengwe, mkifanya hivyo mtapata tabu sana, ” aliwashauri Mexime.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa BancABC, Boniface Nyoni, amesema wao kama wadhamini, wataendelea kufanya kazi zao kwa ushirikiano mkubwa  na vyombo vya habari na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
Michuano hii ambayo ilishirikisha timu nane za Simba, Azam FC, Mtibwa, Polisi Morogoro, Super Falcon, Mtende, Zimamoto na Jamhuri, inatarajiwa kufikia tamati Jumamosi.
Bingwa wa michuano hiyo, atajinyakulia kitita cha sh mil. 40; wa pili sh mil. 20 na waliotinga nusu fainali kila mmoja sh mil. 15 na waliosalia sh mil 5 kila mmoja

Comments