MSONDO, SIKINDE KUPAMBANA IDDI MOSI LEADERS CLUB


 MSONDO NGOMA
SIKINDE NGOMA YA UKAE

Na Mwandishi Wetu
Bendi zenye upinzani wa jadi nchini kama ule wa Simba na Yanga, Msondo Ngoma Music Band na  Mlimani Park Orchestra (Wana Sikinde Ngoma ya Ukae)  zitapambana siku ya Iddi Mosi kwenye viwanja vya Leaders Club, Kinondoni.
Tayari mashabiki wa bendi hizo wameanza maandalizi ya kuzishangilia bendi zao.
Mpambano huo umeandaliwa na kampuni za Keen Arts na kudhaminiwa na kinywaji cha Konyagi.
Mratibu wa mchuano huo Joseph Kapinga amesema pambano hilo litakuwa la kusherekea sikukuu ya Iddi na kuamua ni bendi gani bora kati ya magwiji hao wawili wa muziki wa dansi nchini kwa mwaka 2012.
Kapinga alisema ili kuondoa malamiko ya kuhujumiwa, kila bendi itatumia jukwaa lake kwa kupiga kwa muda wa saa moja kabla ya nyingine kupanda jukwani.
“Litakuwa pamabano la aina yake ukizingatia kuwa itakuwa ni mara ya kwanza kwa bendi hizi pinzani kupambana siku ya sikukuu ya Iddi tangu zianzishwe” alisema Kapinga.
“Pia itakuwa ni mara ya kwanza kwao kushindana katika viwanja vya Leaders Club.”
Kapinga alisema kampuni yake inafanya mipango ya kuwasafirisha wapenzi wa bendi hizo kutoka kila wilaya ya Dar es Salaam kuja kushuhudia mpambano huo.
Alisema mchuano huo itaanza saa nane mchana hadi liamba.
Mwaka jana bendi hizo zilipambana vikali kwenye ukumbi wa TCC Club sikukuu ya Krismasi ambapo mbali na muziki safi na vituko vya hapa na pale kama ilivyo kawaida, zilitoka sare kwa kupata pointi sawa.
Mratibu amesema kuwa mwaka huu mshindi ni lazima apatikane hata kwa kurusha shilingi.

Comments