JK, KAGAME WAIALIKA YANGA IKULU


Mwenyekiti wa Yanga, Yusuf Manji (kati) akizungumza na waandishi wa habari jan akuhusiana na ziara yao nchini Rwanda, kushoto ni makamu mwenyekiti wa Yanga Clement Sanga na kulia ni Katibu wa Yanga, Mwesiga Selestine.

WAKATI mabingwa wa Kombe la Kagame, Yanga, wakiondoka nchini jana kwenda Rwanda kwa mwaliko wa Rais wa nchi hiyo, Meja Jenerali Paul Kagame, Rais Jakaya Kikwete ‘JK’ naye amewaalika Ikulu kuwapongeza.
Rais Kagame, ametoa mwaliko huo kuwapongeza baada ya kutwaa kombe hilo Julai 28, jijini Dar es Salaam, ambako leo hii watamtembelea Ikulu jijini Kigali kwa mujibu wa ratiba.
Kagame, ndie amekuwa mfadhili wa michuano hiyo tangu mwaka 2002, akitoa kiasi cha dola 60,000 kila mwaka kwa ajili ya zawadi ya mshindi wa kwanza hadi wa tatu.
Mwenyekiti wa Yanga, Yusuf Manji, alisema jijini Dar es Salaam jana kwamba, wanashukuru kupata mialiko hiyo ya marais na baada ya kurejea kutoka Rwanda, watapanga siku ya kwenda kumuona JK kwa pongezi.
Alisema, pamoja na mwaliko huo, hawana budi kuwashukuru Watanzania kwa michango na hamasa yao, iliyowezesha Yanga kutwaa ubingwa wa Kagame kwa kishindo, wakiwafunga Azam mabao 2-0.
Kwa ubingwa huo, Yanga imeweka rekodi ya kuubeba mara tano kama ilivyo kwa AFC Leopards ya Kenya tangu kuasisiwa kwa michuano hiyo mwaka 1974.
Wakiwa Rwanda, Yanga watacheza mechi tatu za kirafiki na timu za Rayon, Polisi na nyingine itakayojulikana baadaye.
“Mpaka sasa tunafahamu timu mbili na hiyo timu nyingine wanashughulikia wenyeji wetu, Chama cha Soka cha Rwanda (FERWAFA),” alisema Manji.
Aidha, Manji aliongeza kwamba, beki wao mpya Mbuyi Twite aliyekuwa akikipiga APR, wanatarajia kuungana naye Kigali.

Comments