HANSPOPE MWENYEKITI MPYA WA FRIENDS OF SIMBA


MWANACHAMA maarufu wa klabu ya Simba, Zakaria Hanspope amechaguliwa kuwa Mwenyekiti wa kundi la marafiki wa Simba, ‘Firend of Simba’ akichukua nafasi ya Salum Abdallah ‘Try Again’ aliyeliongoza kundi hilo kwa zaidi ya miaka mitano.
Hanspope, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, alichaguliwa katika kikao kilichofanyika juzi, katika hoteli ya JB Delmonte iliyopo katikati ya Jiji la Dar es Salaam.
Akizungumza mara baada ya kuchaguliwa, Hanspope alisema, atajitahidi kufanya kila awezalo, kuhakikisha kundi hilo linafanya kazi kazi kwa kushirikiana na uongozi, kwa lengo la kuleta maelewano yatakayoijenga Simba imara na kuleta burudani kwa wapenzi na mashabiki.
“Sisi ni Marafiki wa Simba, tunachokifanya lazima kiendane na tafsiri ya neno lenyewe na isije ikawa tofauti, kuwa ni maadui wa Simba, naomba ushirikiano wa pamoja kuhakikisha tunafanikisha malengo yetu,” alisema Hanspope.
Mbali na Hanspope, wengine waliochaguliwa ni Adam Mgoy (Makamu Mwenyekiti), Mulamu Ng’hambi (Katibu Mkuu), Katibu msaidizi ni Niki Magariza huku Juma Pinto ni msemaji wa kundi hilo.
Awali, mmoja wa waasisi wa kundi hilo, Jaji mstaafu Thomas Mihayo, alisema mwelekeo na dira ya kundi hilo lilipotea, hivyo kuwa na imani kwa viongozi wapya kufanya kazi ambayo itakuwa na faida kwa maendeleo ya Simba.
Jaji Mihayo alisema, kundi hilo limekuwa na malengo mazuri, lakini kinachokwamisha sasa hivi ni wanachama wake kutokuwa wamoja na kuwataka kurudisha umoja na kufuatialia mambo ambayo yanapangwa kwa ajili ya utekelezaji.
Mbali ya Salim ambaye katika uongozi wake alileta mafanikio makubwa ndani ya klabu ya Simba, kwa uhamasishaji wa kundi hilo lilijizolea umaarufu mkubwa ndani ya klabu hiyo, viongozi wenginge wa zamani ni Johnson Masabala (Makamu Mwenyekiti), na Issa Batenga aliyekuwa katibu wa kundi hilo.


Comments