BAHANUZI ATUA KWA KAGAME,YANGA KUWAVAA POLISI KESHO


WAKATI mfungaji bora wa  klabu bingwa ya soka Afrika Mashariki na Kati ‘Kombe la Kagame’  Yanga SC, Said Bahanuzi ‘Spider Man’ akitua nchini Rwanda leo, mabingwa hao kesho watashuka katika Uwanja wa Nyamirambo Kigali, Rwanda kuikabili Polisi ya huko katika mchezo wa kujipima nguvu. 
Bahanuzi  hakuwemo katika msafara wa Yanga uliokwenda nchini Rwanda katikati ya wiki iuliyopita kwa mwaliko wa Rais wa nchi hiyo Paul Kagame kwa ajili ya kuwapongeza kutokana na kutwaa ubingwa wa Kagame iyoutwaa kwa mara ya pili mfululizo wiki mbili zilizopita, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kwa kuifunga Azam FC mabao 2-0, kutokana na kuwa na matatizo ya kifamilia. 
Akizungumza kwa simu kutoka Rwanda, Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Yanga Abdallah Binkleb alisema kwamba, Bahanuzi aliwasili huko kutokea Dar es Salaam na kuungana na wenzake ambapo kama kocha ataridhika na kiwango chake  huenda leo akacheza  mechi yao dhidi ya maafande.
 Alisema timu yao ambayo jana  ilianza vema mechi zake za kujipima nguvu nchini humo baada ya kuichapa Rayon Sport mabao 2-0 kwenye Uwanja wa Amahoro mjini Kigali, pamoja na ushindi huo ilipoteza mabao mengi ya wazi baada ya washambuliaji wake kushindwa kutumia vema nafasi za wazi  walizotengeneza. 
Binkleb alisema katika mchezo wao huo  na Rayon, mabao ya Yanga yalipachikwa na Hamisi Kiiza katika dakika  ya pili ya mchezo huo na  Simon Msuva aliyefunga la pili katika dakika ya 12.

Akizungumzia mchezo wao wa kesho na Polisi, Binkleb alisema anaamini timu yao itatoka tena kifua mbele kwani jana kocha wake mkuu, Mbelgiji Tom Saintfiet alifanyia kazi mapungufu yaliyojitokeza juzi hivyo anaamini kitashuka kikosi bora zaidi. 
Aliongeza kuwa, mchezo wa leo utahitimisha ziara yao huko iliyoanza katikati ya wiki iliyopita abapo keshokutwa  wanatarajiwa kurejea jijini Dar es Salaam keshokutwa kuendelea na maandalizi mengine ya ligi kuu soka Tanzania Bara inayotarajiwa kuanza Septemba 15. 
Pamoja na michezo hiyo, Yanga ilipata kuzuru makumbusho ya Kimbari ambayo walizikwa wahanga waliofariki katika mauaji yaliyotokea nchini humo mwaka 1994 kutokana na ugombi wa kikabila.

Yanga pia ilipata fursa ya kutembea Ikulu ya Rwanda na kuonana na Rais Kagame ambapo walizungumza maswala mbalimbali ikiwemo mikakati ya kuendeleza uhusiano mzuri wa kimichezo baina yao. 
Katika ziara hiyo, Yanga inaongozwa na Mwenyekiti Yussuf Manji, Makamu Mwenyekiti, Clement Sanga na Wajumbe wa Bodi ya Wadhamini Mama Fatma Karume, Francis Kifukwe na Seif Ahmed ‘Magari’ pamoja na  Wajumbe wa Kamati ya Utendaji, Abdallah Bin-Kleb na Salum Rupia, huku viuongozi wa benchi la ufundi ni kocha mkuu; Tom Saintfiet, Kocha Msaidizi Fred Felix Minziro, Kocha wa makipa, Mfaume Athumani, Meneja Hafidh Saleh, Daktari, Sufiani Juma na Mtunza vifaa Mahmoud Omary. 
Kwa upande wa wachezaji ni makipa: Yaw Berko, Ally Mustafa ‘Barthez’ na Said Mohamed. Mabeki Shadrack Nsajigwa, Godfrey Taita, Juma Abdul, Oscar Joshua, Stefano Mwasyika, David Luhende, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kelvin Yondan, Ibrahim Job, Ladisalus Mbogo; viungo Athumani Iddi ‘Chuji’, Juma Seif ‘Kijiko’, Salum Telela, Simon Msuva, Shamte Ally, Omega Seme, Idrisa Rashid, Nizar Khalfan, Haruna Niyonzima, Frank Domayo, Rashid Gumbo, Nurdin Bakari na washambuliaji; Hamis Kiiza ‘Diego’, Jerry Tegete na Didier Kavumbangu.

Comments