WATANZANIA WATAKIWA KUUDHAMINI UTAMADUNI WAO

Msanii wa Ras Innocent Nganyagwa akiwasilisha mada kwenye Jukwaa la Sanaa wiki hii. Kushoto kwake ni Afisa Habari Mkuu BASATA Bi Agnes Kimwaga.

Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Habari kutoka Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) Godfrey Lebejo akisisitiza jambo wakati akihitimisha programu ya Jukwaa la Sanaa wiki hii.

Na Mwandishi Wetu 
Watanzania wametakiwa kuuenzi utamaduni wa makabila ambao una thamani kubwa sana, wito huu umetolewa wiki hii kwenye ukumbi wa BASATA na mwanamuziki mkongwe wa regge nchini na mtafiti mbobevu wa masuala ya historia za jamii, Innocent Nganyagwa,  alipokuwa akiwasilisha mada katika Jukwaa la Sanaa kuhusu Umuhimu wa Utafiti Wa Makabila Katika Kuendeleza Utamaduni Wetu.

Alisema tamaduni za makabila mengi ya Tanzania zina mashiko mazuri na yenye thamani ambayo yakienziwa na kuendelezwa, yatawasidia watu katika maendeleo ya sasa.

Alisema Watanzania tunapaswa kujitambua na kujua mashiko ya Sanaa na tamaduni zetu na kuhuisha thamani ya maadili yetu kitaifa.

“Kila kabila lilikuwa na taratibu zake na mifumo yake ya utawala na shughuli zake za uchumi, pia makabila mbalimbali yalishirikiana, mambo haya yakiendelezwa ni dhahiri tunaweza kuendela zaidi katika zama za sasa za changamoto za utandawazi, uliorahisisha maendeleo lakini pia ukatuletea baadhi ya tamaduni za kigeni zinazopotosha maadili.

Msanii huyu aliwataka Watanzania kufanya tafiti zaidi na kujitambua wao ni nani na asili yao ni nini ili wasitegemee historia zilizoandikwa na wageni peke yake, kwani nyingi zinaishia katika mazungumzo waliyopewa bila kushiriki kikamilifu katika kupata taarifa zaidi za historia hizo kwa kuzipima katika ‘mzania jumuishi’ wenye kina kirefu cha mila na desturi.

Nae Kaimu Katibu Mtendaji wa BASATA, ndugu Lebejo, alisistiza kuwa tungeendeleza kilichopo kwenye tamaduni zetu na kukichanganya na teknolojia tungefika mbali sana katika kila eneo, tushikilie mila zetu tusiige vya Wazungu kwani wao wana mila zao na wanaziendeleza kwa mujibu wa mashiko yao ya utamaduni wao, tusibweteke na kupenda vya kuiga vya kigeni wakati tuna mambo yetu mengi yenye thamani na mafundisho ya kuishi maisha sadifu ya kimaadili.
“Tujitambue na kuzifahamu mila zetu kwa kufanya tafiti, tusisubiri mpaka tuwe maprofesa ili kuweza kufahamu tulikotoka, kwani mengi kati ya yanayohusu utamaduni wetu yanatuzunguka katika maisha yetu ya kila siku. Ni suala tu la kuwa na mtazamo chanya na kuamua kwa dhati kuuenzi utamaduni wetu”,alisisitiza ndugu Lebejo.

Comments

  1. Kweli aiyethamini utamaduni wake ni mtumwa wa utamaduni wa wenzake anaouthamini

    ReplyDelete

Post a Comment