TWANGA PEPETA KUPAMBA MISS SINZA 2012

Warembo wa Redds Miss Sinza wakiwa mazoezini kwenye ukumbi wa Mawela social (Ten Star Lounge) uliopo karibu na hotel ya Vatican chini ya mwalimu wa, Mwajabu Juma ambaye anashikiria taji la Top Model . Warembo hao watapanda jukwaani Julai 13 kutafuta tiketi ya kuiwakilisha Sinza katika mashindano ya  Kanda ya Kinondoni na baadaye Miss Tanzania. (Picha na Mpiga Picha wetu)



Na Mwandishi Wetu
WAKATI bendi ya African Stars (Twanga Pepeta) itapamba shindano la kumsaka mrembo wa Redds Miss Sinza 2012 lillopangwa kufanyika Ijumaa kwenye ukumbi wa Mawela Social (Ten Star Lounge) uliopo karibu na hotel ya Vatican City, Kamati ya Miss Tanzania kesho itatembelea warembo hao  kwa lengo la ‘kuwafunda’  tayari kupanda jukwaani.
Mratibu wa kampuni  ya Calapy Entertainment, Majuto Omary alisema jana kuwa Twanga Pepeta imeandaa zawadi kwa mashabiki wake na wale wa urembo kwa kuwapa uhondo wa nyimbo mbili mpya ambazo zitakuwa zinasikika kwa mara ya kwanza jukwaani.
Nyimbo hizo ni Mapambano ya Maslahi uliotungwa na Muumin Mwinjuma, Shamba la Twanga ambao umetungwa na Greyson Semsekwa na mmoja ambao haujapewa jina uliotungwa na Jumanne Saidi ambaye amfunga ndoa na mnenguaji wa bendi hiyo, Asha Sharapova.
Alisema kuwa nyimbo hizo ni zawadi kwa mashabiki wa Twanga wa Sinza na vitongoji  vyake  kwani bendi hiyo haijafanya shoo huko muda mrefu.
“Tunatarajia kuwa na shoo nzuri kutoka kwa warembo na bendi ya Twanga Pepeta ambayo mwaka huu imeshinda tuzo mbili katika tuzo za muziki Tanzania,” alisema.
Kuhusiana na ziara ya Kampuni ya Lino International Agency, Majuto alisema kuwa Lundenga na wenzake watafanya mazungumzo na warembo hao baada ya mazoezi yao ya pamoja.
Alisema kuwa ziara hiyo ni moja ya faraja kwa warembo na kamati ya Miss Sinza kutokana na ukweli kuwa ujio wao ni wa Baraka na hitimisho la mashindano ya vitongoji nchini.
“Miss Sinza ndiyo inafunga pazia la mashindano ya Vitongoji (vituo) nchini, Lundenga na wenzake wanakuja kutoa baraka zao kabla ya kuanza pilikapilika za Redds Miss Tanzania,” alisema.
Shindano hilo lililodhaminiwa na Redds Premium Cold, Dodoma Wine, Kidoti Fashion, Clouds Entertainment, sufianimafoto.blogspot.com, Lady Pepeta na flexi P, Fredito Entertainment, Screen Masters, Brake  Point na Jackz Cosmetics Kinondoni.

Comments