TUKUYU STARS 'BANYAMPALA' KUFUFULIWA UPYA


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

          Tukuyu stars ni timu pekee yenye historia ya aina yake nchini Tanzania. Ilipanda daraja mwaka 1985, ikachukua  ubingwa mwaka 1986, ikashuka daraja mwaka 1987, ikapanda tena daraja mwaka 1988 na baada ya misimu kadhaa ikashuka daraja na kupotea katika ramani ya mpira nchini.  Hii ni historia ya pekee , lakini cha kukumbukwa zaidi ilikuwa ni uwezo wa kusakata soka la nguvu, kasi, akili na ubunifu wa wachezaji   chini ya mwalimu Athuman Juma ( marehemu).
          Kutokana na mwenendo na uwezo wa Tukuyu stars, timu hii ilivuta mashabiki wengi kila kona ya nchi  na Duniani. Hivyo wadau, wapenzi na watu wengine walioguswa na kupotea kwa Tukuyu stars kwenye ramani ya soka nchini wameanzisha mkakati wa kuifufua na kuirejesha Tukuyu stars kwenye ramani ili tuendelee kupata ladha tuliyoikosa, yaani zile burudani za akina Selemani Mathew, Karabi Mrisho, Stephen Mussa ( marehemu), Salum Kabunda Ninja (marehemu), Ally Kimwaga, John Alex, Richard Lumumba, Aston Pardon na wengineo. Hivyo lengo ni kuifufua na kurekebisha mfumo wa uendeshaji wa timu uwe wa kisasa hasa kampuni ili iwe endelevu, shindani na inayojitegemea kiuchumi na kimaamuzi. Kwa maana hiyo wadau, wapenzi na wengine wote wanaoguswa na kutokuwepo kwa Tukuyu stars mnaalikwa kujumuika kwenye mpango huu.
          Katika kufikia malengo yaliyowekwa wadau wameanza utekelezaji wa mpango huu katika ngazi mbalimbali ikihusisha wadau waliopo Dar es salaam na wale waliopo Mbeya.
i)                  Vikao vya wadau waishio Dar es salaam vimeanza na vinaendelea kila ijumaa kuanzia saa kumi na nusu jioni Kinondoni Mkwajuni, Katumba bar. Mada kuu ikiwa ni namna bora ya kuifufua na kuirejesha Tukuyu stars.
ii)               Wadau wa Tukuyu stars waliopo Mbeya wanaendelea na vikao vya kufanikisha siku rasmi ya kongamano la kufufuka kwa Tukuyu stars.
iii)            Ili kuleta hamasa na kuibua vipaji vitakavyounda Tukuyu stars ijayo ligi ndogo imeanzishwa Wilayani Rungwe mahali ilipozaliwa timu hii. Ligi hii inategemea kukamilika yaani Fainali zake kuwa tarehe 04/08/2012
          Siku ya fainali yaani tarehe 04/08/2012 inatarajiwa kuwa siku  ya kujadili na kufufuka rasmi kwa Tukuyu stars, hii ni siku muhimu na inatarajiwa kuwa na matukio mengi na ya kusisimua.  Kutakuwa na michezo mitatu ya utangulizi kabla ya mchezo wa fainali, pia kutakuwa na ngoma za asili maarufu kama  Ing’oma.  Michezo itakuwa kama ifuatavyo:-
i)                  Mechi ya awali ya vijana chini ya miaka 14 ( under 14) walioalikwa wakishindana na wenyeji
ii)               Mechi ya vijana chini ya miaka 17 ( under 17) itafuatia, pia ikihusisha timu waalikwa watakaoshindana na wenyeji.
iii)            Baada ya mechi hizo zitafuatia ngoma za asili
 (Mang’oma)
iv)            Itafuatia mechi ya kukata na shoka ya wakongwe  (veterans )waliochezea Tukuyu stars na timu zingine waliopo Dar es salaam chini ya mwalimu Kennedy Mwaisabula ‘’mzazi’’  wakishindana na wakongwe wenzao (veterans) waliopo Mbeya wakiongozwa na Jimmy Mored na Alex Mwambipile
v)               Baada ya mechi ya Veterans itafuatia fainali ya ligi inayoendelea, ili kumpata bingwa wa mashindano yaliyoanza June.
          Kilele cha shughuli hii kitahitimishwa kwa kongamano kubwa la kuifufua rasmi Tukuyu stars, mjadala huu utahusisha kuona namna bora ya kuendesha timu, na kama ni kampuni basi uuzaji wa hisa utaanza siku hiyo kwa kuorodhesha majina ya wote wanaopenda kununua hisa za kampuni na kujadili namna ya upatikanaji wa Bodi ya timu na watendaji wa timu. Katika kongamano hili zitatolewa tuzo rasmi kwa waanzilishi na viongozi wa Tukuyu stars, wanaotegemewa kupewa tuzo ni kama Ramnik Patel Kaka (muasisi), mzee Kasyupa (katibu mkuu wa kwanza), mzee Malakasuka, aliyekuwa mkuu wa mkoa  wa Mbeya Major General (mstaafu) Rashid Nalihinga Makame , mzee Mwakasala na wale wote waliojitoa kwa hali na mali kuifanya Tukuyu stars ing’are katika medani ya soka.
Pia vitakabidhiwa vifaa vya awali kwa ajili ya kuanza rasmi kambi ya timu ya Tukuyu stars.
          Maandalizi ya timu ya veterans waliopo Dar es salaam yanatarajia kuanza siku ya jumamosi na kusimamiwa na mwalimu Kennedy Mwaisabula katika viwanja vya Harbours Pub kurasini kuanzia saa mbili asubuhi.  Wachezaji wanaotarajiwa kucheza mechi hiyo na kuanza mazoezi ni:-
Godwin Aswile ‘’Mlimba’’ ‘’Scania’’ ( Baba  Subi), Seleman Mathew,Karabi Mrisho,Salum Kussi,Asanga Aswile, Mbwana  Makata,Peter Mwakibibi, Sekilojo Chambua, Nsajigwa Mwaisaka,Geofrey Amanyisye,Ezekiel ( Masatu),Shedrack Nsajigwa Fusso, Christopher Michael, Lawrence Mwalusako, John Mwansasu, Deo Philip Masanja, Michael Mbaruku, Ally Kassimu,  Nsangalufu Joseph.

Kupitia taarifa hii tunawaalika wachezaji na wadau wote wanaopenda kushiriki  kwenye mazoezi na kucheza mechi hii  wafike jumamosi asubuhi  saa mbili katika viwanja vya Harbours pub.
          Vikao vya mikakati ya kufufua Tukuyu stars vinaendelea kila ijumaa saa kumi na nusu jioni kinondoni Mkwajuni Katumba bar hivyo wapenzi na wadau  wote mnaalikwa ili tuweze kupanga kwa pamoja, pia tujadili namna ya kusafiri kwenda Tukuyu Mbeya kwa ajili ya hiyo siku rasmi.
          Michezo inaburudisha, inatoa ajira, inajenga undugu na zaidi ya hapo inawafanya wanajamii wasahau tofauti zao na kuungana kusonga mbele katika maendeleo yao. Tunawaombeni wadau wote wenye mapenzi mema na Tukuyu stars tuungane ili turudishe heshima ya miaka ya 1980  wakati Tukuyu stars ikipambana na Simba ya Dsm, Yanga ya Dsm, Pamba ya Mwanza, Ushirika ya Moshi, Mecco ya Mbeya, Coastal Union ya Tanga, Nyota Nyekundu ya Dsm, Sigara ya Dsm, Pilsner ya Dsm, Lipuli ya Iringa na timu nyingine. Tujumuike ili tuzalishe wachezaji mahiri kama Justin Nicodemus Mtekele ( marehemu), Aston Pardon, Sekilojo Chambua, Hussein Zito, Stephen Mussa ( marehemu),  Jabir Mohamed       ( marehemu), Peter Mwakibibi na wengine wengi.

Comments