Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea kwa
masikitiko taarifa za kifo cha mjumbe wake wa Kamati ya Nidhamu na Usuluhishi,
Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Shabani Semlangwa kilichotokea Julai 5 mwaka
huu kutokana na maradhi.
ACP Semlangwa ambaye alizikwa juzi (Julai 6 mwaka huu)
katika Kijiji cha Gumba, Wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani alitoa mchango mkubwa
akiwa mjumbe wa Kamati hiyo inayoongozwa na Kamishna wa Polisi (CP) mstaafu
Alfred Tibaigana.
Msiba huo ni pigo kwa familia ya ACP Semlangwa, TFF na
familia ya mpira wa miguu kwa ujumla nchini kutokana na mchango na mawazo
aliyotoa kwa shirikisho akiwa mjumbe wa kamati hiyo.
TFF inatoa pole kwa familia ya marehemu ACP Semlangwa, jamaa
na marafiki na kuwataka kuwa na uvumilivu katika kipindi hiki cha msiba huo
mzito. Pia TFF itatoa ubani wa sh. 200,000 kwa familia ya marehemu kama rambirambi zake.
Mungu aiweke roho ya marehemu ACP Shabani Semlangwa mahali
pema peponi. Amina
Comments
Post a Comment