MTANZANIA KUZIPIGA NA MGANDA IBF

Shauri katikati akiwa na Madaraka Nyerere kushoto na promota Rutainurwa kulia
Na Prince Akbar
SHIRIKISHO la Ngumi la Kimataifa (IBF) limetangaza rasmi mpambano kati ya bondia Ramadhani Shauri wa Tanzania na Sande Kizito kutoka Uganda. Mpambano huo utafanyika kutafuta bingwa wa “IBF Continental Afrika” katika uzito wa Unyoya (Featherweight) kilo 58 katika ukumbi wa Diamond Jubilee jijini Dar-Es-Salaam.
Bondia Ramadhani Shauri anatoka katika kundi la kocha Mzazi lenye makao yake makuu Ubungo katika eneo la Mabibo. Shauri ana rekodi ya mapabano 12 ambapo katika maisha yake ya ngumi ameshinda mara 11na kupoteza mara 1. Naye bondia Sande Kizito ana rekodi ya mapambano 12 ambapo ameshinda mapamambano 7 na kupoteza 9.
Aidha, bondia Nasibu Ramadhani atapambana na bondia Twalibu Mubiru toka Kenya kugombea mkanda wa “IBF East & Central Africa” katika uzito wa Bantam. Nassibu Ramadhani ana rekodi ya mapambano 9 na kupoteza mara 2 wakati Twalib Mubiru ana rekodi ya mapambano 11 amepoteza mara 7 na kutoka draw mara 2.
Mpambano kati ya Ramadhani Shauri na Sande Kizito unafanyika wakati Tanzania ikijijenga katika medani ya michezo ya kimataifa. Tayari Rais Jakaye Mrisho Kikwete ameshakutana na viongozi wa vyama na taasisi mbalimbali za michezo kujadili programu za kuiendeleza michezo hapa Tanzania.
Promota wa mpambano huo mkubwa uliopewa jina la “The Rumble in the City” ni mfanyabiashara maarufu katika jiji la Dar-Es-Salaam Lucas Rutainurwa wa kampuni maarufu ya Kitwe General Traders ya jijini Dar-Es-Salaam.
Kampuni hii ndiyo iliyopromoti mpambano mwingine wa IBF mwezi wa Aprili ambapo ulimshughudia bondia machachari wa Tanzania anayejiita kuwa mbunge wa Rorya kwa wakazi wa jimbo hilo wanaoishi katika jijini Dar-Es-Salaam Manda Maugo akipoteza katika raundi ya nane!
Nalo Shirikisho la Ngumi la Kimataifa (IBF) lilizindua program maalum ya “Utalii wa Michezo” katika mkutano wake wa 29 uliofanyika mwezi wa Juni uliofanyika katika jijini la Honolulu jimbo la Hawaii nchini Marekani ambayo imelenga kuinua mchezo wa ngumi katika bara la Afrika wakati nchi za Ghana na Tanzania ni nchi za mfano (Pilot Countries).
Katika programu hii ya “Utalii wa MIchezo” IBF mbali na kuwapa nafasi mabondia kadhaa toka Tanzania na Ghana kugombea mikanda mbalimbali itaendesha pia programu ya mikutano yake hapa Tanzania na kuwaleta wanachama wake kupanda wa mlima Kilimanjaro kila mwaka. Programu hii itawaleta watalii wengi nchini Tanzania na kutangaza vivutio vya kitalii kupitia michezo.
Tayari bondia Helen Joseph wa Ghana anategemea kupanda ulingoni Agosti 11 kupambana na bondia Dahianna Santana wa Dominican Republic kugombea mkanda wa dunia katika uzito wa unyoya (Featherweight) upande wa wanawake. Mpambano huo utafanyika wiki mbili kabla ya mpambano wa Ramadhani Shauri ya Sande Kizito.
Wakati huo huo promota wa mpambano huo bwaan Lucas Rutainurwa akizungumza na mwandishi wa habari hii alisema kuwa ameamua kuwekeza katika “Utalii wa Michezo” ili kuwawezesha vijana kujiajiri na kujenga uchumi wa nchi ya Tanzania.
Rutainurwa alisema kuwa ana ratiba ya mapambano ya ubingwa wa Afrika kila baada ya miezi miwili mwaka huu na mwak akesho ambayo itaipa Tanzania nafasi ya kunyanyua medani ya michezo pamoja na kuwawezesha vijana kujiajiri.
Ameziomba kampuni pamoja na watu wenye mapenzi mema kujitokeza kwa wingi kusaidia kufadhili mapamnano haya ili kuiwezesha Tanzania kuinuka kimichezo.

Comments