MCHAKATO UCHAGUZI DRFA KUANZA JULAI 15


Kamati ya Uchaguzi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imeridhia ombi la Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) kuanza mchakato wa uchaguzi wake Julai 15 mwaka huu. 
DRFA iliwasilisha ombi TFF ili kusogeza mbele kuanza kwa mchakato huo kwa vile Katiba yao ambayo waliagizwa na Kamati ya Uchaguzi ya TFF kuifanyia marekebisho kabla ya kuingia kwenye uchaguzi huo bado iko kwa Msajili. 
Awali DRFA ilikuwa ianze mchakato wa uchaguzi Julai Mosi mwaka huu. Kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi za Wanachama wa TFF, mchakato wa uchaguzi unatakiwa kuchukua siku 40 tangu kuanza kutolewa fomu kwa wagombea hadi siku yenyewe ya uchaguzi. 
Pia Kamati ya Uchaguzi ya TFF imekubali ombi la Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Kigoma (KRFA) kuanza mapema mchakato wa uchaguzi wake. Sasa mchakato wa uchaguzi wa chama hicho utaanza Septemba Mosi mwaka huu badala ya Septemba 15 mwaka huu kama ilivyokuwa imepangwa awali.

Comments