MAKINDA YA NIGERIA YATUA, KUWAVAA NGORONGORO HEROES J'2


Timu ya Taifa ya vijana wenye umri chini ya miaka 20 ya Nigeria (Flying Eagles) inatarajia kuwasili nchini leo (Julai 25 mwaka huu) saa 10 jioni kwa ndege ya RwandAir ikiwa na msafara wa watu 30 wakiwemo wachezaji 18.

Flying Eagles itapambana na Ngorongoro Heroes katika mechi ya kwanza ya raundi ya pili itakayofanyika Jumapili (Julai 29 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 10 kamili jioni.

Mechi hiyo ya kuwania tiketi ya kucheza fainali za 18 za Afrika kwa vijana wenye umri chini ya miaka 20 zitakazochezwa mwakani nchini Algeria itachezeshwa na waamuzi kutoka Kenya wakati Kamishna ni Charles Masembe kutoka Uganda.

Flying Eagles inayofundishwa na kocha John Obuh, jana (Julai 24 mwaka huu) ilicheza mechi ya kirafiki na Rwanda (Young Amavubi) kwenye Uwanja wa Amahoro jijini Kigali. Nigeria ililala bao 1-0.

Msafara wa timu hiyo unaongozwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Ufundi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Nigeria (NFF), Chris Green. Baadhi ya wachezaji walioko katika kikosi cha Flying Eagles ni Chidi Osuchukwu, Alhaji Gero, Shehu Abdullahi, Aminu Umar, Aliyu Mohamed, Uche Agbo, Jonah Usman, Harrison Egbune, Hassan Abubakar na Yahya Adamu.

Viingilio katika mechi hiyo vitakuwa sh. 3,000 kwa viti vya rangi ya chungwa, bluu na kijani wakati VIP B na C itakuwa sh. 5,000. Kiingilio kwa VIP A itakuwa sh. 10,000.

Comments