KIPIGO CHA SIMBA CHAZUA GUMZO BUNGENI


KIPIGO cha mabao 3-1 ilichokipata timu ya Simba kutoka kwa timu ya Azam katika michuano ya Kombe la Kagame, kiliibua mjadala mzito bungeni kwa mashabiki wa klabu hiyo kupigwa vijembe na wenzao wa Yanga.
Shabiki mkubwa wa Simba, Profesa Juma Kapuya ambaye pia ni Mbunge wa Urambo Magharibi, ndiye alianza kuchokoza mjadala pale alipoitwa na Mwenyekiti wa Bunge ili awasilishe taarifa ya Kamati yao ya Miundombinu.
Prof. Kapuya baada ya kufika mbele, alisimama na kutaka kuanza kuzungumza bila kuwasha kipaza sauti, akidai rangi yake nyekundu ambayo inatumiwa na klabu yake kuwa inamchanganya, jambo lililoibua vicheko kwa wabunge wenzake.
Hata hivyo, baada ya kipindi cha maswali na majibu kwisha wakati wa asubuhi, Mwenyekiti wa Bunge, Jenista Mhagama, aliwatambulisha wageni na kutoa matangazo ya kazi kisha akawaambia wabunge kuwa ana tangazo fupi kwao.
“Waheshimiwa wabunge nataka kuwajulisha kuwa Kampuni ya Azam ina bidhaa nyingi na nzuri, hivyo mnashauriwa kutumia bidhaa hizo kwa kuwa ni imara na bora, maana hata mashabiki wa Simba wanajua kwamba Azam ni kiboko,” alisema Mhagama na kuibua vicheko kwa wabunge.
Hata hivyo Profesa Kapuya alipomaliza kusoma taarifa ya kamati, alihitimisha kwa vijembe kwa watani zao wa Yanga akisema: “Nawapongeza Simba kwa kucheza vizuri japo wamefungwa na Azam, lakini wamekubali, hawajawa kama wenzetu waliofungwa goli tatu na timu hiyo halafu wakapigana…na sasa wamepewa jina la ‘HU HAA’.

Comments