HABARI NJEMA KWA WANAYANGA

Kiungo wa Kimataifa raia wa Rwanda,Haruna Niyonzima Fabregas amerejea jana usiku na kujiunga na Kikosi cha Mabingwa wa Afrika Mashariki na Kati Young Africans Sport Club (YANGA) katika mazoezi yanayotarajiwa kuanza leo jioni saa kumi katika uwanja wa Kaunda Jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na tovuti ya klabu   www.youngafricans.co.tz kiungo huyo amesema kuchelewa kwake kulitokana na matatizo binafsi yaliyokuwa yamemkuta wakati akiwa nchini kwao na kusababisha kuchelewa kujiunga na Kikosi chake.
Haruna amewataka wachezaji wenzake kurejesha heshima kwa mara nyingine kwa kutwaa kombe la Kagame katika michuano inayotarajiwa kuanza Julai 14 Mwaka huu, huku Yanga ikiwa ndiyo Mabingwa watetezi wa michuano hiyo.
Niyonzima amesema tangu alipokuwa mapunziko alikuwa akifuatilia kwa karibu juu ya Klabu yake ya Yanga hasa katika zoezi la usajiri unaoendelea na kupongeza usajili huo kutokana na baadhi ya wachezaji anaowafahamu kusajiriwa katika kikosi hicho.
Yanga itaanza kutupa karata yake dhidi ya Atletico ya Burundi ambapo mechi hiyo ndiyo itakayokuwa ni pekee wakati wa ufunguzi itachezwa katika uwanja wa Taifa,Jijini Dar es Salaam huku Simba ikaanza kampeni siku inayofuata.
Mabingwa hao watetezi kundi lake limejumuisha na timu za Wau Salaam ya Sudan,Altetico ya Burundi na APR ya Rwanda.
Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa BARAZA la vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), Nicholous Musonye amesema mpaka sasa mdhamini ni mmoja aliyejitosa kwenye michuano hiyo ambaye ni Rais wa Rwanda,Paul Kagame.
Jumla ya timu 12 zitashiriki katika michuano hiyo ambayo itaanza Julai 14 hadi Julai 28 ambapo wawakilishi hao watatoka katika nchi za Tanzania,Uganda,DR Congo,Djibout,Zanzibar,Kenya,Sudan Kusini,Rwanda na Burundi.(Mwandishi wetu Louis Sendeu)

Comments