AZAM YAITOA SIMBA



Shujaa wa leo, John Bocco 'Adebayor' habari picha kwa hisani ya http/bongostaz.blogspot.com'


Na Prince Akbar
AZAM imefuzu kuingia Nusu Fainali ya Klabu Bingwa ya soka Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame, baada ya kuifunga Simba SC mabao 3-1, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam jioni hii na sasa itamenyana na AS Vita ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) keshokutwa.
Shujaa wa Azam leo alikuwa John Raphael Bocco ‘Adebayor’ aliyefunga mabao yote hayo, moja kipindi cha kwanza na mengine kipindi cha pili.
Lakini japokuwa Bocco aliondoka na mpira leo, lakini nyota wa mchezo anastahili kuwa Salum Abubakar ‘Sure Boy Jr’, ambaye alitawala sehemu ya kiungo na kuiongoza vema timu yake hata ikapata ushindi huo mnono.
Bocco, mfungaji bora wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, alifunga bao la kwanza dakika ya 17, akiunganisha krosi ya nyota kutoka Ivory Coast, Kipre Herman Tcheche, wakati bao la pili alifunga dakika ya 46, baada ya kupewa pasi na Sure Boy na la tatu alifunga dakika ya 73.
Kabla ya Bocco kufunga bao la kuununua mpira uliotumika katika mechi ya leo, Shomari Kapombe kwa juhudi zake binafsi aliifungia Simba bao la kufutia machozi dakika ya 53.
Ikumbukwe jana APR na Yanga zilikuwa za kwanza kujikatia tiketi ya Nusu Fainali, baada ya kuzitoa Mafunzo na URA.
Katika Robo Fainali ya tatu leo, AS Vita imeingia Nusu Fainali, baada ya kuifunga Atletico kwa mabao 2-1. Taddy Etekiama aliifungia Vita dakika ya sita na Pierre Kwizera akasawazisha dakika ya 48, kabla ya Basilua Makola kufunga la ushindi dakika ya 90+2.
Sasa Nusu Fainali zote zitafanyika keshokutwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Azam wakianza na Vita na baadaye Yanga na APR saa 10:00 jioni.
Katika mchezo wa leo, kikosi cha Azam kilikuwa; Deo Munishi, Ibrahim Shikanda, Erasto Nyoni, Said Mourad, Aggrey Morris, Kipre Michael Balou/Ramadhan Chombo, Kipre Herman Tcheche/George Odhiambo ‘Blackberry’, Salum Abubakar, John Bocco, Ibrahim Mwaipopo na Khamis Mcha ‘Vialli’/Jabir Aziz.
Simba SC; Juma Kaseja, Haruna Shamte, Shomary Kapombe, Lino Masombo, Juma Nyosso, Mussa Mudde, Uhuru Suleiman/Kiggi Makassy, Mwinyi Kazimoto, Felix Sunzu, Haruna Moshi na Jonas Mkude/Amri Kiemba

Comments