SIMBA SC KUIVAA EXPRESS YA UGANDA BILA NYOTA WAKE WAANDAMIZI


WAKATI kikosi cha mabingwa watetezi wa ligi kuu soka Tanzania Bara Simba kikitarajiwa kuondoka jijini kesho kwenda mkoani Mwanza, uongozi umewapa mapumziko mafupi nyota wake waandaamizi wanaokipiga katika timu ya Taifa ‘Taifa Stars’. 
Nyota hao ni pamoja na Nahodha Juma Kaseja, Haruna Moshi ‘Boban’, Mwinyi Kazimoto na Amir Maftah ambao walirejea nchini juzi kutoka Msumbuji walipokwenda kucheza na wenyeji wao ‘Mambaz’ katika mchezo wa kuwania kufuzu fainali za Afrika (AFCON) zitakazopigwa mwakani nchini Afrika Kusini, ambapo ilitolewa kwa mikwaju ya penalty. 
Ofisa habari wa Simba Ezekiel Kamwaga alisema jana kwamba wameawapa mapumziko nyota hao ili kujiweka sawa kwani wamekuwa wakitumika kwa muda mrefu. 
Alisema kutokana na mapumziko hayo, kwenda kwao itategemea na utashi wao wenyewe na kwamba hata mechi za kanda ya ziwa hawatashiriki kuzicheza. 
“Ni kwamba tumeamua kuwapa mapumziko nyota hawa lakini kama watapenda kwenda Mwanza wataamua wenyewe lakini huko hawataweza kucheza ile michezo ya kirafiki zaidi ya kushiriki katika hafla za kutembeza kombe,”alisema. 
Simba ambayo inakwenda huko kwa lengo la kupeleka ubingwa kwa mashabiki wa kanda ya Ziwa jumamosi itacheza na mabingwa wa ligi kuu soka nchini Uganda, Express jumapili katika uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga, huku Jumamosi itakipiga na Toto African katika uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.

Kikosi cha Simba kinaendelea na mazoezi kwenye uwanja wa TCC Chang’ombe chini ambapo mazoezi hayo yanahusisha wachezaji wa kikosi cha kwanza na wale wa timu ya Vijana.

Comments