KOCHA MPYA WA TIMU YA TAIFA YA VIJANA ATAMBULISHWA


Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limemtambulisha rasmi leo mbele ya waandishi wa habari kocha mpya wa timu za Taifa za vijana, Jakob Michelsen kutoka Denmark ambaye amechukua nafasi ya Kim Poulsen ambaye hivi sasa anainoa Taifa Stars. 
Michelsen ambaye amepewa mkataba wa mwaka mmoja alitambulishwa na Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah na kusema falsafa yake ni kama ile ya Poulsen ya kumiliki mpira na kushambulia muda wote wa mchezo.
Kabla ya kuja Tanzania, Michelsen alikuwa kocha wa timu ya daraja la kwanza ya Hobro IK ya Denmark. Ana leseni A ya ukocha kutoka Shirikisho la Mpira wa Miguu Ulaya (UEFA), leseni ya ukocha wa vijana kutoka Chama cha Mpira wa Miguu cha Denmark (DBU). 
Moja ya mafanikio yake ni kuipa ubingwa wa Denmark, timu ya Skovbakken kwenye ligi ya timu zenye umri chini ya miaka 18. Ubingwa huo aliupata msimu wa 2005/2006.

Comments