DIWANI DOTTO MGENUI RASMI MISS KIGAMBINI CITY 2012


Na Mwandishi Wetu
DIWANI wa Kata ya Kigamboni kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM), Dotto Msawa, atakuwa mgeni rasmi katika shindano la urembo la kitongoji cha Kigamboni mwaka huu ' Redd's Miss Kigamboni 2012' ambalo litafanyika kesho Ijumaa kwenye ukumbi wa Navy Beach jijini Dar es Salaam.
Akizungumza jana jijini, Mratibu wa shindano hilo, kutoka kampuni ya K&L Media Solutions, Somoe Ng'itu, alisema jana kuwa maandalizi ya zoezi hilo yamekamilika na wanamshukuru diwani huyo pamoja na diwani wa Vijibweni (CCM), Suleiman Mathew, kusaidia maandalizi ya shindano hilo.
Alisema kuwa warembo 12 kutoka sehemu mbalimbali hapa nchini wanatarajia kuchuana kuwania taji hilo na anaamini kwamba kitongoji hicho kimepania kurudisha taji la Miss Tanzania kwenye Kanda ya Temeke.
Aliongeza kuwa ili kuboresha shindano hilo bendi ya muziki wa dansi ya FM Academia maarufu Wazee wa Ngwasuma na msanii na mchekeshaji mahiri hapa nchini, Mpoki watatumbuiza kwenye kinyang'anyiro hicho.
Aliwaomba mashabiki na wadau wa sanaa ya urembo kujitokeza kushuhudia malkia wa Kigamboni anavyopatikana ikiwa ni shindano pekee lililoko ufukweni wa bahari.
Aliwataja warembo watakaochuana kuwa ni pamoja na Susanne Jeremiah, Agness Goodluck, Elizabeth Boniface, Dorothea Kessy, Esther Albert, Edda Silyvester, Sophia Martin, Doreen Kweka, Khadija Kombo, Linnah David, Rosemary Peter na Domotila Shayo.
Aliwashukuru wadhamini ambao wamejitokeza kusaidia shindano hilo ambao ni Redd's, Dodoma Wine, hoteli ya Hope Country, Screen Masters, Global Publishers, Nobro Collections, Times FM na Clouds FM.
Aliongeza kuwa warembo watakaoshika nafasi tatu za juu kutoka katika shindano hilo wataungana na wenzao kutoka vitongoji vya Kurasini na Chang'ombe ili kuwania taji la Kanda ya Temeke baadaye mwaka huu.

Comments