UONGOZI YANGA KUJADILI ILIVYOVURUNDA VPL


KAMATI ya utendaji ya klabu ya Yanga inatarajiwa kukutana kesho kwa ajili ya kujadili ripoti ya kamati ya ufundi ya timu hiyo, imefahamika. 
Mwenyekiti wa Yanga Lloyd Nchunga ameiambia mamapipiro blog kwamba kwamba kamati ya mashindano chini ya mwenyekiti wake Mohammed Bhinda inatarajiwa kukutana jioni ya leo kwa ajili ya kuandaa ripoti hiyo. 
Alisema kuwa  mara baada ya kupitia na kuijadili ripoti hiyo ndipo hatua nyingine zitafuata kabla ya kuziwasilisha rasmi kwa wanachama wa klabu hiyo. 
Nchunga na kamati nzima ya utendaji ya Yanga ilijikuta katika wakati mgumu hivi karibuni baada ya timu hiyo kuonyesha mwenendo mbaya wa ligi hiyo na hatimaye kupoteza ubingwa wake iliyokuwa ikiushikilia. 
Yanga ambayo ilimaliza ligi hiyo ikiambulia nafasi ya tatu ikiwa na pointi 49 juzi ilimaliza ligi hiyo kwa kupokea kipigo cha mabao 5-0 toka kwa mahasimu wao wa jadi Simba ambao walitwaa ubingwa. 
Kufanya vibaya kwa Yanga katika ligi kuu kulipelekea baadhi ya wanachama kuutaka uonmgozi ujiuzulu,ambapo Nchunga aliwataka wanachama kusubiri ligi imalizike kwanza na uongozi ufanye tathmini ndipo wachukue hatua zinazostahili. 
Aidha, katika sekeseke hilo wajumbe wawili wa kamati ya utendaji Sarah Ramadhan na Seif Ahmed walitangaza kuachia ngazi, pia mjumbe wa kamati ya usajili na mashindano ya klabu hiyo Abdallah Binkleb naye kujiengua. 
Kama hiyo haitoshi, Baraza la wazee wa klabu hiyo lilitangaza kuichukua timu wiki moja kabla ya kumalizika kwa ligi kwa madai kuwa walikubaliana na Nchunga, lakini baadaye mwenyekiti huyo alikana suala hilo na kusema kuwa hawezi kukabidhi timu kwa watu asiokuwa na uhakika nao. 
Kauli hiyo ya Nchunga iliwachukiza wazee hao ambao waliamua kumvulia kofia Nchunga huku wakidai kusikitishwa na kauli za fedheha ambazo zilikuwa zikitolewa na Nchunga dhidi yao . 

Comments