SIMBA WASAKA VIDEO ZA WASUDAN


WAWAKILISHI wa Tanzania kwenye Kombe la Shirikisho barani Afrika, (CAF) timu ya Simba wameanza kusaka mikanda ya video ya wapinzani wao kwenye kombe hilo, Al Ahly Shandy ya Sudan.
Simba na Al Ahly Shandy zitakwaana Aprili 29 kwenye uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Habari zilizopatikana leo toka ndani ya klabu hiyo zinasema kwamba kazi ya kusaka kanda hizo wamempa mmoja ya wachezaji aliyewahi kukipiga Simba aliyepo nje ya nchi.
Mmmoja ya viongozi wa Simba aliuambia mtandao huu kwamba wameamua kusaka kanda hizo ili wafanyie kazi mbinu za wapinzani wao hao.
Alisema wameamua kusaka kanda za wapinzani hao kutokana na kutoifahamu vema timu hiyo hivyo wanaamini kanda hizo zitawasaidia kwa kiasi kikubwa.
Tayari kikosi cha Simba kimeingia kambini jioni ya leo katika hoteli ya Bamba Beach iliyopo Kigamboni jijini Dar es salaam kujiandaa pia na michezo yake ya ligi kuu soka Tanzania bara ambapo jumapili hii itakwaana na maafande wa Ruvu Shooting katika uwanja wa Taifa.

Comments